Posts Tagged ‘CUF’
Azimio la Mtwara -Uwajibikaji katika Uvunaji wa Maliasili ya Nchi yetu
Azimio la Mtwara
Uwajibikaji katika Uvunaji wa Maliasili ya Nchi yetu.
Tanzania kama zilivyo nchi nyingi za bara la Afrika imejaaliwa kuwa na Rasilimali mbali mbali za asili. Miongoni mwa rasilimali hizo ni pamoja na Madini na Gesi Asilia. Usimamizi wa uvunaji wa rasilimali hizi umegubikwa na manung’uniko makubwa ya wananchi hususan kutokana na usiri mkubwa uliopo kwenye mikataba ya uvunaji wa Maliasili hizi za Taifa. Mikataba yote 6 ya uvunaji wa Dhahabu bado ni Siri kubwa na vile vile mikataba yote 26 ya utafutaji na uvunaji wa Gesi Asilia na Mafuta. Mikataba miwili imevuja mpaka sasa na yote imeonyesha tofauti kubwa sana na mikataba ya mfano ambayo Serikali imeweka wazi. Mikataba ya mfano hutumika kujadiliana na makampuni ya uwekezaji katika utafutaji na uchimbaji wa Gesi na Mafuta hapa nchini. Mageuzi katika sekta ndogo ya gesi na mafuta yamekuwa hayashirikishi wananchi na hufanywa kwa usiri mkubwa na hivyo kusababisha wananchi kutokuwa na taarifa kabisa na kinachoendelea katika utajiri wao wa asili.
Mwaka 2007 nilitangaza Azimio la Songea lililokuwa na malengo makuu manne
1) kutokuwa na mikataba mipya ya madini mpaka mikataba iliyokuwepo ipitiwe. Mikataba yote ya madini ilipitiwa na Kamati ya Bomani na tangu mwaka 2007 hapajawa na mkataba Mpya wa madini ulioingiwa na Serikali.
2) kufanya mabadiliko ya sheria zote za kodi ambazo ni kikwazo katika kukusanya kodi katika sekta ya madini. Sheria husika zimefanyiwa marekebisho ikiwemo kupandisha mrahaba, kufuta nafuu ya kodi ya ongezeko la thamani kwa kampuni za madini na kuirejesha kodi ya ongezeko la mtaji.
3) Serikali kumiliki sehemu ya hisa katika migodi ya madini. Kwa mujibu wa sera Mpya ya madini ya mwaka 2009 na sheria Mpya ya madini ya mwaka 2010 Serikali itakuwa na hisa katika kila mgodi Mpya unaoanza nchini.
4) Halmashauri za Wilaya zenye migodi kupata mgawo wa theluthi ya mrahaba unaokusanywa katika madini yanayovunwa nchini. Pamoja na kwamba hivi sasa Halmashauri zinakusanya kodi ya ‘ cess’ lakini bado Serikali Kuu inabeba fedha yote ya mrahaba.
Malengo haya yaliongoza mjadala wa masuala ya madini mwaka 2007 mpaka 2010 sheria Mpya ya madini ilipotungwa. Utekelezaji wa Azimio la Songea ni wa zaidi ya 75% lakini bado kilio cha wananchi kipo pale pale. Hii inatokana na usiri mkubwa wa mikataba na hususan mikataba ya gesi na miundombinu yake. Usiri huu unasababisha ukosefu mkubwa wa uwajibikaji kwa upande wa watendaji wa Serikali. Usiri hupelekea rushwa na ufisadi. Moja ya sababu kubwa zinazotolewa na watetezi wa usiri wa mikataba ni kwamba mikataba ile ina Siri za kibiashara na hivyo washindani wa kibiashara wataiba Siri za wenzao. Hoja hii ni nyepesi sana kwani makampuni yote makubwa yanayowekeza nchini yamesajiliwa katika masoko ya hisa kwenye nchi za magharibi na katika masoko hayo mikataba yao hulazimika kuwekwa wazi. Hivyo usiri huo ni kwa wananchi tu na sio kwa hao washindani. Makampuni mengi yaliyopo nchini yanamilikiwa na watu wale wale kupitia masoko ya hisa. Vile vile majirani zetu kama Msumbiji wameweka mikataba yao yote wazi.
Ni dhahiri kwamba moja ya sababu kubwa ya kushamiri kwa rushwa nchini kwetu ni ukosefu wa mfumo thabiti wa uwajibikaji. Ndio maana katika mkutano wa kufunga mwaka 2014 na kuukaribisha mwaka 2015 uliofanyika mjini Mtwara tarehe 31 Desemba 2014, niliwaomba wananchi wa Mtwara kuufanya mwaka 2015 kuwa ni mwaka wa kuwajibishana. Hivyo Azimio la Mtwara ni wito wa kutaka Uwazi na Uwajibikaji katika utafutaji na uvunaji wa mali asili za nchi yetu. Azimio la Mtwara lina malengo yafuatayo
1 kutaka mikataba yote inayohusu uvunaji wa rasilimali za nchi iwekwe wazi kwa wananchi na Bunge liipitie kuidhia kabla ya kuingiwa kwa mikataba hiyo
2 kutaka haki ya wananchi kuruhusu utafutaji wa madini au gesi na mafuta katika maeneo yao ( right of free prior informed consent )
3 kutaka sehemu ya mrahaba unaotokana na uvunaji wa Maliasili ya nchi kugawanywa kwa maeneo yanayovunwa rasimali hizo
4 kutaka mfumo wa mapato na matumizi ya mapato yasiyo ya kikodi ( rents ) yanayotokana na uvunaji wa Maliasili za nchi kuwa wazi kwa wananchi na kushirikisha wananchi katika kupanga matumizi husika kwa faida ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo
Azimio hili ni wito tu utakaotusaidia kuiwajibisha Serikali katika masuala ya utajiri wa Taifa.
Zitto Kabwe, Mb
Mtwara 31-12-2014
RUZUKU YA VYAMA VYA SIASA
Shilingi bilioni 67.7 zimelipwa na Serikali kwa vyama vya siasa katika kipindi cha miaka 4, 2009/2010 mpaka 2012/2013. Fedha hizi hazijakaguliwa kwa mujibu wa Sheria.
Mahesabu ya Vyama vya siasa nchini yanapaswa kukaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Mahesabu ya Serikali kwa mujibu wa Sheria tangu mwaka 2009. Tangu mwaka huo Kamati ya PAC haijawahi kuona Taarifa ya CAG kuhusu ukaguzi wa vyama vya siasa. Nilihoji tangia Aprili 2011 https://zittokabwe.wordpress.com/category/ruzuku-vyama-vya-siasa/
Kamati imemwita Msajili wa vyama ili kufafanua ni kwa nini Vyama vya Siasa nchini havifuati sheria (vifungu vya sheria vimeambatanishwa hapa chini). Uvunjifu huu wa Sheria ni wa makusudi au wa kutokujua? Sheria inataka Mahesabu ya vyama yatangazwe kwa uwazi, tena kwa Government Notice. Umewahi kuona? Tarehe 15 Oktoba, 2013 Kamati ya PAC itatafuta majibu haya kutoka kwa Msajili na ikibidi vyama vyenyewe. Tunataka uwazi wa matumizi ya Fedha za Umma.Vyama vya siasa ndio vinaunda Serikali, uwazi unaanzia huko ili kuepuka fedha chafu kama za EPA kuingia kuvuruga uchaguzi.
Vyama vifuatavyo vimepokea Ruzuku ya jumla shilingi bilioni 67.7 tangu mwaka wa fedha 2009/2010;
- CCM tshs 50.97 bilioni
- CHADEMA tshs 9.2 bilioni
- CUF tshs 6.29 bilioni
- NCCR – M tshs 0.677 bilioni
- UDP tshs 0.33 bilioni
- TLP tshs 0.217 bilioni
- APPT – M tshs 11 milioni
- DP tshs 3.3 milioni
- CHAUSTA tshs 2.4 milioni
Political Parties Act, No. 5 of 1992 as ammended from time to time.
14. -(1) Every political party which has been fully registered shall—
a) maintain proper accounts of the funds and property of the party;
b) submit to the Registrar –
“(i) an annual statement of the account of the political party audited by the Controller and Auditor-General and the report of the account.” (This became law in March, 2009)
ii) an annual declaration of all the property owned by the party.
(2) The Registrar, after inspecting any accounts or report submitted pursuant to this section may, for the benefit of the members or the public, publish any matter relation to the funds, resources or property of any party or the use of such funds, resources or property.
(3) The Registrar shall publish in the official Gazette, an annual report on the audited accounts of every party.
18. -(1) Subventions granted to a party may be spent only on
(a) the parliamentary activities of a party;
(b) the civil activities of a party;
(c) any lawful activity relating to an election in which a party nominates acandidate;
(d) any other necessary or reasonable requirement of a party.
(2) Subventions granted to a political party shall be accounted for to the Registrar, separately from the accounting for other funds of the party.
(3) Any party which fails or neglects to account for subventions in accordance with this Act, shall forfeit the right to any subsequent subvention due to the party in accordance with this Act.
(4) Where the Registrar is for any reasonable cause, dissatisfied with any account of subventions submitted by any party, so much of the subvention which has not been accounted for or has not been accounted for satisfactorily, shall be deducted form any subsequent subvention due to the party.
(5) If by reason of failure to submit an account or for any other reason, the Registrar has reason to suspect that any offence under the Penal Code may have been committed in relation to the money which has not been committed in relation to the money which has not be been accounted for, he may make a report to a police station, and the officer in charge of that police station shall cause the matter to be investigated.
18A. Notwithstanding the provisions of sections 14 and 18, every political party receiving subvention in accordance with this Act shall, not later than 3151
October every year, submit to the Registrar financial statements and audited accounts reflecting any other source of funds and details regarding the manner in which such funds were used.” (became law in 2009)
Muswada wa Marekebisho ya Katiba ujenge Mwafaka wa Kitaifa
Zitto Kabwe[1], Mb
Kama kuna jambo moja ambalo huunganisha Taifa ni Katiba ya Taifa hilo. Katiba huweka misingi mikuu ya nchi na namna ya kujenga na kuendesha Taifa. Hivyo Katiba inapaswa kuwa ni matokeo ya mwafaka wa kitaifa kwenye masuala yote ya msingi ya nchi husika. Tanzania imekuwa ikiongozwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 kama ilivyofanyiwa marekebisho mara kwa mara. Kabla ya hapo kulikuwa na Katiba ya Uhuru ambayo ilitokana na Mwafaka wa wapigania Uhuru wa nchi yetu, baadaye Katiba ya Jamhuri ya Tangayika na kisha Katiba ya muda ya Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kabla ya kubadili jina na kuitwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Ukiachana na Katiba ya Uhuru, Katiba nyingine zote hazikutokana na mwafaka wa kitaifa bali matakwa ya tabaka la watawala. Katiba ya kudumu ya mwaka 1977 ni zao dhahiri kabisa la utawala wa chama kimoja ambacho kilikuwa na dhamira ya kushika hatamu za uongozi. Kutokana na hali hii haikuchukua muda kwa wasomi mnamo mwaka 1983 kuanza harakati za kuifanyia mabadiliko makubwa. Mabadiliko hayo yalizaa kuwemo kwa Haki za Msingi za Binaadamu katika Katiba katika mabadiliko ya mwaka 1984, miaka saba tu toka kuandikwa kwa Katiba ya kudumu.
Takribani mwaka mzima huu kumekuwa na madai ya kuandikwa kwa Katiba mpya. Madai haya sio mapya kwani huibuka na kusinyaa kila baada ya uchaguzi Mkuu. Itakumbukwa kwamba miaka ya Tisini mwishoni kundi la vyama vya siasa liliunda Kamati ya Mabadiliko ya Katiba (KAMAKA) ili kudai kuandikwa kwa Katiba mpya. Hata hivyo safari hii sauti ya mabadiliko imekuwa ni kubwa sana kiasi cha Serikali kusikia na hivyo kupeleka Bungeni muswada wa Marejeo ya Katiba kwa lengo la kuandika Katiba mpya ya nchi yetu. Muswada huu umeleta kelele nyingi na manung’uniko mengi sana kutoka kwa makundi mbalimbali ya jamii kuanzia vyama vya siasa, viongozi wa dini na Asasi za Kijamii. Baadhi ya Asasi za Kijamii zimeunda Jukwaa la Katiba ili kuweza kuratibu vizuri juhudi za kuandikwa kwa Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Sababu kubwa ya kupingwa kwa muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya mwaka 2011 ni kwamba mchakato umewekwa kwenye Dola mno na hasa kwenye Urais. Rais anateua Tume ya kukusanya maoni, Rais anateua Bunge la Katiba nk. Watu wengi tungependa kuona mchakato unakuwa kwa wananchi zaidi. Serikali imefanya marekebisho kadhaa na kupanua wigo wa mjadala wa Katiba na pia kumhusisha kikamilifu Rais wa Zanzibar katika mchakato.
Baadhi yetu tunaona kama nafasi ya Zanzibar katika mchakato imepewa nguvu kubwa kupita kiasi. Ninadhani Zanzibar inastahili kupata nafasi hii katika mchakato wa Katiba. Jambo ambalo ni vizuri tulitilie maanani ni kwamba Muungano wa Mwaka 1964 ulihusisha nchi mbili huru zenye hadhi sawa mbele ya sheria za kimataifa. Linapokuja suala la kuandika Katiba ya Muungano, pande mbili za Muungano zinakuwa na hadhi sawasawa. Kwamba Zanzibar ishiriki kwenye masuala ya Muungano tu ni hoja inayojadilika iwapo tu Katiba ya Muungano ingetofautisha kinagaubaga taasisi za kimuungano na zisizo. Kwa mfano Sura ya Bunge katika Katiba ni lazima ijadiliwe na pande zote mbili ingawa Bunge wakati mwingine hupitisha miswaada ambayo sio ya masuala ya Muungano. Aina ya Muungano wetu inatulazimisha kufanya hivi tunavyofanya sasa. Mkataba wa Muungano ni lazima uheshimiwe kama ulivyo sasa.
Katiba mpya yaweza kuweka makubaliano mapya lakini muswada wa sasa ni lazima utambue nafasi halali ya Zanzibar kwa mujibu wa Katiba ya sasa na Hati za Muugano. Suala hili ni suala la kisheria na sio suala la idadi ya watu au ukubwa wa eneo la nchi husika. Nchi ya Ushelisheli yenye watu 80,000 ina nafasi sawa na Tanzania yenye watu 42 milioni katika SADC, AU na UNO. Zote zina kura moja tu. Huu ndio ukweli na hatuna budi kukubaliana nao.
Muswada unampa mamlaka Rais wa Tanzania na Rais wa Zanzibar kuteua Tume ya Katiba. Tume hii maRais hawatapata ushauri wa mtu mwingine yeyote kwa mujibu wa kifungu cha (6) na vifungu vidogo (1), (2) na (3). Wanasiasa wakiwemo Wabunge, Wawakilishi, viongozi wa vyama wa Ngazi za Taifa, Mkoa au Wilaya hawatakuwa na sifa za kuteuliwa.
Inawezekana kabisa waandishi wa muswada walikuwa na mantiki ya kuuondoa mchakato kwenye mikono ya wanasiasa. Nia hii njema haikufikiriwa vizuri hata kidogo. Njia hii haijengi mwafaka. Tume hii sio ya Wataalamu, ni Tume inayopaswa kuwa na sura ya kitaifa. Nafasi ya wanasiasa katika mchakato wa kukusanya maoni ni muhimu sana katika kuhalalisha mchakato wenyewe. Tume lazima ionekane ni Tume ya Taifa na sio Tume ya maRais. Hivyo kipengele hiki cha kuwanyima sifa wanasiasa kinapaswa kufutwa katika muswada. Wabunge na Wawakilishi kwa kuwa ni sehemu ya Bunge la Katiba wasiwemo katika Tume, lakini viongozi wengine wa kisiasa wawe na haki ya kuteuliwa kuwa wajumbe.
Lakini pia Rais ateue Tume kutokana na maoni kutoka katika makundi yenye maslahi ya karibu na Katiba ya nchi na hivi ni vyama vya siasa. Ninapendekeza kwamba katika Wajumbe 30 wa Tume ya kukusanya maoni ya Katiba, 10 watokane na vyama vya siasa vyenye Wabunge kwa uwiano wa CCM 2, CHADEMA 2, CUF 2, NCCR 2, TLP 1 na UDP 1. Kila chama cha siasa chenye Wabunge kupitia kiongozi wake Bungeni kipeleke majina ya watu wanaowapendekeza kuwa katika Tume ya Katiba na kutokana na Mapendekezo hayo Rais atawateua kuwa wajumbe. Masharti mengine ya nusu kutoka kila upande wa Muungano yazingatiwe.
Muswada unapendekeza kuwepo kwa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Tume. Kifungu cha cha 7 kifungu kidogo (1), (2) na (3) kinaweka utaratibu wa kupatikana kwa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Tume. Muswada unasema UTEUZI wa Mwenyekiti na Makamu utazingatia kwamba mmoja atoke uapnde mmoja wa Muungano na mwingine upande wa Pili wa Muungano. Ingawa Muswada hausemi waziwazi lakini ni dhahiri kwamba Mwenyekiti wa Tume atateuliwa na Rais baada ya kushauriana na kukubaliana na Rais wa Zanzibar. Sitaki kujenga hoja kwamba Mwenyekiti na Makamu wachaguliwe na wajumbe wa Tume kutoka miongoni mwao lakini ni dhahiri Mwenyekiti wa Tume anapaswa kuwa mtu mwenye heshima kubwa hapa nchini. Ningependekeza kwamba maRais wateue Wenyeviti wenza badala ya Mwenyekiti na Makamu wake ili kuweka nafasi sawa kwa pande mbili za Muungano. Hapa nchini tunao Watanzania ambao wamefanya kazi iliyotukuka katika nyadhifa mbalimbali na sasa ni wastaafu wasio na nia yeyote ya madaraka ya kisiasa wanaoweza kuongoza vizuri kabisa Tume hii. Ni pendekezo langu kwamba Dkt. Salim Ahmed Salim na Jaji Joseph Sinde Warioba wawe wenyeviti wenza wa Tume ya Katiba. Uzoefu wao katika uongozi na kuijua kwao nchi kutasaidia sana kuhakikisha kwamba mchakato wa kukusanya maoni na kisha kuandika Katiba unakuwa na mafanikio kwa kuzingatia misingi ya Taifa letu.
Muswada unapendekeza kwamba Hadidu rejea za Tume zitolewe na maRais. Kifungu cha nane na muswada kuhusu hadidu rejea nadhani hakina mantiki sana. Madhumuni ya muswada yanasema pamoja na mambo mengine muswada unaweka masharti kuhusu Hadidu rejea za Tume. Wakati huo huo muswada unasema Hadidu rejea zitakuwa ni hati ya kisheria itakayozingatiwa na Tume katika kazi zake.
Mantiki ni kwamba Hadidu rejea zinapaswa kuwa sehemu ya Muswada kama ‘schedule’ ili kuzipa nguvu ya kisheria badala ya tangazo katika gazeti la Serikali. Hadidu rejea zikiwa ni sehemu ya Muswada zitajadiliwa na Bunge na kupitishwa hivyo kuwa ni jambo ambalo limefikiwa kwa mwafaka wa wawakilishi wa wananchi.
Muswada unataka uamuzi wa kura ya maoni kuhusu Katiba uwe ni kukubaliwa na nusu ya Watanzania katika kila upande wa Muungano. Nadhani hapa tunacheza na Katiba ya nchi. Katiba ya nchi inapaswa kukubaliwa na theluthi mbili ya wapiga kura wa pande zote za Muungano yaani kila upande theluthi mbili. Hii itaipa Katiba ‘legitimacy’ na hivyo kuheshimiwa na wananchi na watawala. Kuna woga gani uliopo kutaka katika ikubalike na nusu ya wapiga kura? Mifano ya nchi nyingi duniani Katiba inapaswa kukubaliwa na theluthi mbili ya wapiga kura. Hata jirani zetu wa Kenya ilikuwa hivyo na hata kura ya maoni kuhusu mwafaka huko Zanzibar ilikuwa hivyo. Kwa kuwa Katiba ni chombo cha mwafaka wa kitaifa, muswada utamke kwamba Katiba mpya itakuwa imepita iwapo theluthi mbili ya wapiga kura watapiga kura ya ndio.
mwisho
[1] Zitto Kabwe ni Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kaskazini na Naibu Katibu Mkuu CHADEMA. Maoni haya ni maoni binafsi ya Zitto na kwa vyovyote vile hayawakilishi msimamo rasmi wa CHADEMA au Kambi ya Upinzani Bungeni.