Zitto na Demokrasia

Zitto na Demokrasia

Posts Tagged ‘CUF

Call fresh elections in Zanzibar

with 3 comments

Call fresh elections in Zanzibar

Call for fresh elections

Call for fresh elections

ACT Wazalendo is a party that stands firm on democracy and the due process that comes with it, steadfast in ensuring that the voice of the people is heard and adhered too without compromising on the principles of democracy.

What has transpired in Zanzibar has left us both in awe and disgust on how certain individuals can manipulate the system to best suite their crude desire for power. Right after the nullification of the elections in Zanzibar, ACT Wazalendo was firm in its stand that democracy was being toyed with and that the Zanzibari peoples wishes were not respected. It is the party’s firm belief that Maalim Seif Sharif Hamad was the chosen president for the people and by the people.

We raised ten (10) points of caution to President Magufuli; as the custodian of democracy in the United Republic of Tanzania for him to take to task, one of them being the current situation in Zanzibar showing all signs of lacking any democratic decorum. This plea unfortunately fell on deaf ears and the outcome of this negligence was the re-run of the Zanzibar election in March, which to date still bids the question of the legality and mannerism of how it was conducted.

ACT Wazalendo continues its fight for a booming democratic environment in Zanzibar that would foster the growth of new age politicians who are not intimidated by sheer police brutality or the power of the state. With this stand, ACT Wazalendo, has continually denounced the legality of the election in Zanzibar and has chosen not to recognise the current government of Zanzibar in its totality for, if there is ever a doubt that ones rights are infringed the party will not stand by those who infringing the rights of another.

Chaos breeds fear and fear has no part in the struggle to attain justice. Dr. Shein recently has been quoted saying “I am not afraid of Maalim Seif, for he does not have no posses tanks or ammunition”. In hindsight he is right, Maalim Seif does not possess the power and might of the state, after the sabotage that took place in October 2016 he is merely a citizen and former 2nd Vice president of Zanzibar. But let us not forget that he also happens to be the leader of a group of people on the Isles, maybe he does not require military might to be feared all he needs to do is get the attention of his followers. Maybe this was the trigger effect that made the army interrogate the politician when he simply wanted to practice his democratic right to be heard.

ACT Wazalendo cannot condone the words said by Dr. Shein, for one they are beneath him and beneath any self respecting citizen of the United Republic of Tanzania, we were liberated; one half by good diplomacy and the other half by force. It would be wise for Dr. Shein to remember the seat that he is clinging on comes with its own history, and it should be a lesson to him no to mock the people by threatening them with military might, after all the Sultan of Oman, not only had his army but also the backing of the then hegemony United Kingdom, this did not stop those who could not stand injustice to stand up against military might. Words such as those uttered by Dr. Shein only work to remind us that Zanzibar is not a step sibling that we can ignore, that such mishap and insensitivity from a seasoned politician leaves the isle vulnerable to many a thing, we do not want to see our brothers and sisters shed blood…again.

As a party, ACT Wazalendo is fully aware of the hardship that faces the Zanzibar people, the political tension translates to a stagnant economy and a demoralised society. We do understand that there is a need for the people to take control of their state but we firmly believe and have not lost hope that the process be ballot and not bullet. One way of ensuring that the Zanzibari people walk away the winners and not just the politician, is for those who want to serve the people to lower themselves and consider their people first and not self gratification.

If we may, let us restart the clock again for Zanzibar, go to the ballot and ensure that the peoples wishes are respected no matter what the outcome maybe. Some may argue that how can we restart the clock? That at no point in time can a state be without a leader. For this we say, have a transitional government that comprises of members from all political players on the isles, let that government involve people who are respected by all fractions of Zanzibaris.

Possibly the greatest thing for the Zanzibari people  to do is to ignore the blatant attack on their integrity and rights by Dr. Shein, for he may have not known better. Let history be a reminder for him and a point to remember for the people on the isles that throughout oppressors have met an unfavourable outcomes, we do not wish to see the same for Zanzibar no do we wish for their good name to be tarnished.

Zitto Kabwe, MP

Party Leader, ACT Wazalendo

Written by zittokabwe

June 14, 2016 at 11:45 AM

Azimio la Mtwara -Uwajibikaji katika Uvunaji wa Maliasili ya Nchi yetu

with 5 comments

Azimio la Mtwara

Uwajibikaji katika Uvunaji wa Maliasili ya Nchi yetu.

"Azimio la Mtwara" tarehe 31-12-2014 Zitto Kabwe na Prof. Ibrahim Lipumba

“Azimio la Mtwara” tarehe 31-12-2014 Zitto Kabwe na Prof. Ibrahim Lipumba

Tanzania kama zilivyo nchi nyingi za bara la Afrika imejaaliwa kuwa na Rasilimali mbali mbali za asili. Miongoni mwa rasilimali hizo ni pamoja na Madini na Gesi Asilia. Usimamizi wa uvunaji wa rasilimali hizi umegubikwa na manung’uniko makubwa ya wananchi hususan kutokana na usiri mkubwa uliopo kwenye mikataba ya uvunaji wa Maliasili hizi za Taifa. Mikataba yote 6 ya uvunaji wa Dhahabu bado ni Siri kubwa na vile vile mikataba yote 26 ya utafutaji na uvunaji wa Gesi Asilia na Mafuta. Mikataba miwili imevuja mpaka sasa na yote imeonyesha tofauti kubwa sana na mikataba ya mfano ambayo Serikali imeweka wazi. Mikataba ya mfano hutumika kujadiliana na makampuni ya uwekezaji katika utafutaji na uchimbaji wa Gesi na Mafuta hapa nchini. Mageuzi katika sekta ndogo ya gesi na mafuta yamekuwa hayashirikishi wananchi na hufanywa kwa usiri mkubwa na hivyo kusababisha wananchi kutokuwa na taarifa kabisa na kinachoendelea katika utajiri wao wa asili.

Mwaka 2007 nilitangaza Azimio la Songea lililokuwa na malengo makuu manne

1) kutokuwa na mikataba mipya ya madini mpaka mikataba iliyokuwepo ipitiwe. Mikataba yote ya madini ilipitiwa na Kamati ya Bomani na tangu mwaka 2007 hapajawa na mkataba Mpya wa madini ulioingiwa na Serikali.

2) kufanya mabadiliko ya sheria zote za kodi ambazo ni kikwazo katika kukusanya kodi katika sekta ya madini. Sheria husika zimefanyiwa marekebisho ikiwemo kupandisha mrahaba, kufuta nafuu ya kodi ya ongezeko la thamani kwa kampuni za madini na kuirejesha kodi ya ongezeko la mtaji.

3) Serikali kumiliki sehemu ya hisa katika migodi ya madini. Kwa mujibu wa sera Mpya ya madini ya mwaka 2009 na sheria Mpya ya madini ya mwaka 2010 Serikali itakuwa na hisa katika kila mgodi Mpya unaoanza nchini.

4) Halmashauri za Wilaya zenye migodi kupata mgawo wa theluthi ya mrahaba unaokusanywa katika madini yanayovunwa nchini. Pamoja na kwamba hivi sasa Halmashauri zinakusanya kodi ya ‘ cess’ lakini bado Serikali Kuu inabeba fedha yote ya mrahaba.

Malengo haya yaliongoza mjadala wa masuala ya madini mwaka 2007 mpaka 2010 sheria Mpya ya madini ilipotungwa. Utekelezaji wa Azimio la Songea ni wa zaidi ya 75% lakini bado kilio cha wananchi kipo pale pale. Hii inatokana na usiri mkubwa wa mikataba na hususan mikataba ya gesi na miundombinu yake. Usiri huu unasababisha ukosefu mkubwa wa uwajibikaji kwa upande wa watendaji wa Serikali. Usiri hupelekea rushwa na ufisadi. Moja ya sababu kubwa zinazotolewa na watetezi wa usiri wa mikataba ni kwamba mikataba ile ina Siri za kibiashara na hivyo washindani wa kibiashara wataiba Siri za wenzao. Hoja hii ni nyepesi sana kwani makampuni yote makubwa yanayowekeza nchini yamesajiliwa katika masoko ya hisa kwenye nchi za magharibi na katika masoko hayo mikataba yao hulazimika kuwekwa wazi. Hivyo usiri huo ni kwa wananchi tu na sio kwa hao washindani. Makampuni mengi yaliyopo nchini yanamilikiwa na watu wale wale kupitia masoko ya hisa. Vile vile majirani zetu kama Msumbiji wameweka mikataba yao yote wazi.

Ni dhahiri kwamba moja ya sababu kubwa ya kushamiri kwa rushwa nchini kwetu ni ukosefu wa mfumo thabiti wa uwajibikaji. Ndio maana katika mkutano wa kufunga mwaka 2014 na kuukaribisha mwaka 2015 uliofanyika mjini Mtwara tarehe 31 Desemba 2014, niliwaomba wananchi wa Mtwara kuufanya mwaka 2015 kuwa ni mwaka wa kuwajibishana. Hivyo Azimio la Mtwara ni wito wa kutaka Uwazi na Uwajibikaji katika utafutaji na uvunaji wa mali asili za nchi yetu. Azimio la Mtwara lina malengo yafuatayo

1 kutaka mikataba yote inayohusu uvunaji wa rasilimali za nchi iwekwe wazi kwa wananchi na Bunge liipitie kuidhia kabla ya kuingiwa kwa mikataba hiyo

2 kutaka haki ya wananchi kuruhusu utafutaji wa madini au gesi na mafuta katika maeneo yao ( right of free prior informed consent )

3 kutaka sehemu ya mrahaba unaotokana na uvunaji wa Maliasili ya nchi kugawanywa kwa maeneo yanayovunwa rasimali hizo

4 kutaka mfumo wa mapato na matumizi ya mapato yasiyo ya kikodi ( rents ) yanayotokana na uvunaji wa Maliasili za nchi kuwa wazi kwa wananchi na kushirikisha wananchi katika kupanga matumizi husika kwa faida ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo

Azimio hili ni wito tu utakaotusaidia kuiwajibisha Serikali katika masuala ya utajiri wa Taifa.

Zitto Kabwe, Mb

Mtwara 31-12-2014

RUZUKU YA VYAMA VYA SIASA

with 2 comments

Msajili wa Vyama vya Siasa-Jaji Francis S.K.Mutungi

Msajili wa Vyama vya Siasa-Jaji Francis S.K.Mutungi

Shilingi bilioni 67.7 zimelipwa na Serikali kwa vyama vya siasa katika kipindi cha miaka 4, 2009/2010 mpaka 2012/2013. Fedha hizi hazijakaguliwa kwa mujibu wa Sheria.

Mahesabu ya Vyama vya siasa nchini yanapaswa kukaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Mahesabu ya Serikali kwa mujibu wa Sheria tangu mwaka 2009. Tangu mwaka huo Kamati ya PAC haijawahi kuona Taarifa ya CAG kuhusu ukaguzi wa vyama vya siasa. Nilihoji tangia Aprili 2011 https://zittokabwe.wordpress.com/category/ruzuku-vyama-vya-siasa/

Kamati imemwita Msajili wa vyama ili kufafanua ni kwa nini Vyama vya Siasa nchini havifuati sheria (vifungu vya sheria vimeambatanishwa hapa chini). Uvunjifu huu wa Sheria ni wa makusudi au wa kutokujua? Sheria inataka Mahesabu ya vyama yatangazwe kwa uwazi, tena kwa Government Notice. Umewahi kuona? Tarehe 15 Oktoba, 2013 Kamati ya PAC itatafuta majibu haya kutoka kwa Msajili na ikibidi vyama vyenyewe. Tunataka uwazi wa matumizi ya Fedha za Umma.Vyama vya siasa ndio vinaunda Serikali, uwazi unaanzia huko ili kuepuka fedha chafu kama za EPA kuingia kuvuruga uchaguzi.

Vyama vifuatavyo vimepokea Ruzuku ya jumla shilingi bilioni 67.7 tangu mwaka wa fedha 2009/2010;

  • CCM tshs 50.97 bilioni
  • CHADEMA tshs 9.2 bilioni
  • CUF tshs 6.29 bilioni
  • NCCR – M tshs 0.677 bilioni
  • UDP tshs 0.33 bilioni
  • TLP tshs 0.217 bilioni
  • APPT – M tshs 11 milioni
  • DP tshs 3.3 milioni
  • CHAUSTA tshs 2.4 milioni

Political Parties Act, No. 5 of 1992 as ammended from time to time.

14. -(1) Every political party which has been fully registered shall—
a) maintain proper accounts of the funds and property of the party;
b) submit to the Registrar –

“(i) an annual statement of the account of the political party audited by the Controller and Auditor-General and the report of the account.” (This became law in March, 2009)

ii) an annual declaration of all the property owned by the party.

(2) The Registrar, after inspecting any accounts or report submitted pursuant to this section may, for the benefit of the members or the public, publish any matter relation to the funds, resources or property of any party or the use of such funds, resources or property.

(3) The Registrar shall publish in the official Gazette, an annual report on the audited accounts of every party.

18. -(1) Subventions granted to a party may be spent only on

(a) the parliamentary activities of a party;
(b) the civil activities of a party;
(c) any lawful activity relating to an election in which a party nominates acandidate;
(d) any other necessary or reasonable requirement of a party.

(2) Subventions granted to a political party shall be accounted for to the Registrar, separately from the accounting for other funds of the party.

(3) Any party which fails or neglects to account for subventions in accordance with this Act, shall forfeit the right to any subsequent subvention due to the party in accordance with this Act.

(4) Where the Registrar is for any reasonable cause, dissatisfied with any account of subventions submitted by any party, so much of the subvention which has not been accounted for or has not been accounted for satisfactorily, shall be deducted form any subsequent subvention due to the party.

(5) If by reason of failure to submit an account or for any other reason, the Registrar has reason to suspect that any offence under the Penal Code may have been committed in relation to the money which has not been committed in relation to the money which has not be been accounted for, he may make a report to a police station, and the officer in charge of that police station shall cause the matter to be investigated.

18A. Notwithstanding the provisions of sections 14 and 18, every political party receiving subvention in accordance with this Act shall, not later than 3151
October every year, submit to the Registrar financial statements and audited accounts reflecting any other source of funds and details regarding the manner in which such funds were used.” (became law in 2009)

Mafuta kuwa suala la Muungano tulikosea

with 17 comments

  • Kila upande wa Muungano uchimbe Mafuta na Gesi Asili yake na Mapato yawe ya Serikali ya upande husika.
  • Shughuli za Utafutaji kwenye vitalu vyenye mgogoro ziendelee mara moja
  • Zanzibar ianzishe Shirika lake la Mafuta (PetroZan)
  • Katiba mpya itofautishe utafutaji (upstream) na Biashara (uchimbaji, midstream na downstream)

Moja ya suala linalosubiriwa kwa hamu kubwa katika mjadala na hatimaye uandishi wa Katiba mpya ni suala la Mafuta na Gesi Asilia kuwa jambo la Muungano au liondolewe katika orodha ya mambo ya Muungano. Suala hili limezusha mjadala mkubwa sana mara kwa mara nchini Tanzania kiasi cha lenyewe kuwa ni hoja ya wale wasiotaka tuwe na Dola ya Jamhuri ya Muungano Tanzania.

Wakati Muungano unaanzishwa mwaka 1964 Mafuta na Gesi hayakuwa masuala ya Muungano. Nimeangalia katika Hati ya Muungano ambayo ilikuwa ni sehemu ya Katiba ya Muda ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka 1965, suala hili halikuwamo katika orodha ya mambo Kumi na Moja ya Muungano. Nyaraka nilizoziona zinaonyesha kwamba suala la Mafuta na Gesi Asilia liliongezwa katika orodha ya Mambo ya Muungano mwaka 1968. Kuna watu wanahoji kihalali kabisa kwamba nyongeza ya jambo hili ilifanywa bila kufuata taratibu na hivyo kufanywa kinyemela na kuna wengine wanasema jambo hili lilifuata taratibu zote za kisheria ikiwemo kupigiwa kura na Bunge la Muungano na kuungwa mkono na theluthi mbili ya Wabunge kutoka pande zote za Muungano.

Katika moja ya vikao vya Bunge katika Bunge la Tisa, aliyekuwa Naibu wa Waziri wa Nishati na Madini Ndugu Adam Malima alileta kumbukumbu za mjadala Bungeni (Hansard) za mjadala wa suala la Mafuta na Gesi ili kuthibitisha kwamba jambo hili halikuuingizwa kwenye Katiba kinyemela.

Wakati umefika kwa Watafiti wa Masuala ya Muungano wakapekua nyaraka hizi na kutwambia ukweli ulio ukweli mtupu wa namna suala la Mafuta na Gesi lilivyoingizwa katika orodha ya mambo ya Muungano. Hata hivyo, jambo hili sasa ni jambo la Muungano kwa mujibu wa Katiba na ni dhahiri kuwa WaTanzania wa Zanzibar hawafurahiswhi nalo na hivyo kuazimia kupitia Azimio la Baraza la Wawakilishi kwamba jambo hili liondolewe kwenye orodha ya masuala ya Muungano. Kwa vyovote vile Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inapaswa kutoa uamuzi wa mwisho utakaomaliza mjadala huu.

Jambo la kusikitisha ni kwamba licha ya Bunge la Muungano kuamua kuongeza suala la Mafuta na Gesi asilia katika masuala ya Muungano, mwaka mmoja baada ya uamuzi huo likaundwa Shirika la Maendeleo ya Mafuta Tanzania (TPDC) kwa amri ya Rais wa Jamhuri ya Muungano (establishment order). Shirika hili halikuanzishwa kwa Sheria ya Bunge au kwa Sheria ya Makampuni kama yalivyo Mashirika mengi ya Umma hapa nchini bali kwa amri ya Rais ya mwaka 1960. Katika amri hii ya Rais, Shirika la TPDC halikupewa ‘mandate’ ya kimuungano. Shirika hili mipaka yake ilianishwa kuwa ni Tanzania bara peke yake. Hivyo suala la Muungano likawekewa Shirika la Tanganyika kulisimamia!

Kama ilikuwa ni bahati mbaya au makusudi au kupitiwa kwa viongozi wetu wa wakati huo ni vigumu kujua lakini huu ni mkanganyiko mkubwa ambao ulipaswa kurekebishwa mapema sana.

Shirika la TPDC limekuwa likifanya kazi ya kusimamia Sekta ya Mafuta na Gesi ikiwemo kutoa vibali vya kutafuta mafuta, kuingia mikataba na Makampuni ya kimataifa na kuisimamia mikataba hiyo. Miongoni mwa mikataba hiyo ni kwenye maeneo ambayo kama isingekuwa Muungano yangekuwa ni Maeneo ya Jamhuri ya Watu wa Zanzibar. Mbaya zaidi Mikataba yote ya utafutaji na uchimbaji Mafuta inafanywa inaingiwa na Waziri wa Nishati na Madini Wizara ambayo sio ya Muungano. Hakuna hata eneo moja ambalo taratibu zimewekwa kwamba pale ambapo eneo hilo ni eneo lilikuwa chini ya himaya ya Jamhuri ya Watu wa Zanzibar basi mikataba isainiwe na Mawaziri wawili wa sekta hiyo kutoka kila upande wa Muungano.

Ni dhahiri kwamba kama ni kusahau hapa kulikuwa na kusahau kukubwa ambako hakustahmiliki kwa mtu yeyote mwenye upeo achilia mbali mwananchi wa kawaida wa Zanzibar ambaye anaona anaonewa na kugandamizwa na Bara.

Mnamo miaka ya mwanzo ya 2000, Shirika la TPDC liliingia mikataba ya Vitalu kadhaa vya Mafuta miongoni vya vitalu hivyo ni vitalu nambari 9, 10, 11 na 12 mashariki ya visiwa vya Pemba na Unguja. Vile vile Shirika na Wizara ya Nishati waliingia mkataba mwingine katika Kitalu kilichopo kati ya Pemba na Tanga (mahala ambapo kumekuwa na dalili za wazi za kuwapo Mafuta kutokana na kuonekana kwa ‘Oil sips’ mara kwa mara.

Vitalu 9, 10, 11 na 12 vilipewa kampuni ya Shell ya Uholanzi na kitalu cha kati ya Tanga na Pemba walipewa Kampuni ya Antrim ya Canada ambayo baadaye waliuza sehemu ya Kampuni yao kwa Kampuni ya RAK Gas kutoka Ras Al Khaimah huko United Aarab Emirates. Kwa kuwa Vitalu hivi vipo katika eneo la iliyokuwa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar kabla ya Muungano, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ilikataa shughuli zozote kufanyika mpaka suala la Mafuta na Gesi kuondolewa katika orodha ya Mambo ya Muungano lipatiwe ufumbuzi.

Uamuzi huu wa Serikali ya Zanzibar ni uamuzi ambao ungechukuliwa na Serikali yeyote ile yenye mapenzi ya dhati na watu wake. Uamuzi huu ulileta mjadala mpana sana katika masuala ya Muungano na ambao hawana taarifa waliubeza sana. Hata hivyo suala hili likafanywa ajenda katika vikao vya masuala ya Muungano vinavyoitwa Vikao vya Kero za Muungano. Miaka kumi suala hili linajadiliwa na Maamuzi hayafanyiki! Hivi sasa kila suala lenye kuangukia kwenye Katiba husukumwa huko na hivyo kutoa ahueni kwa wanaogopa kufanya maamuzi.

Katika medani za uchumi kila suala lina muda wake. Masuala ya utafutaji wa Mafuta ni masuala yanayoongozwa na msimu na kuendelea kuchelewa kufanya maamuzi juu ya suala hili kunalitia hasara Taifa, Hasara ya Mabilioni ya Fedha na hasara kubwa zaidi ya kufahamu utajiri uliojificha chini ya Maji ya Bahari inayozunguka Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Hivi sasa Pwani ya Afrika Mashariki inarindima (trending) katika utafutaji wa Mafuta na Gesi asilia. Huko Msumbiji Makampuni mbalimbali yamegundua Gesi asilia nyingi inayofikia zaidi ya futi za ujazo trillion 107 (107TCF) kwa makadirio ya chini. Hapa Tanzania utajiri wa Gesi asilia uliogunduliwa hadi hivi sasa na kutangazwa umefikia futi za ujazo trillion 20 (20TCF) ambazo ni sawa na utajiri wa thamani ya dola za kimarekani trillion 6. Makadirio yanakisiwa kuwa Tanzania kuna  futi za ujazo trillioni 85 (85TCF) za Gesi Asilia katika eneo la Kusini kuanzia vitalu namba 1 mpaka namba 5 ikiwemo vitalu vya nchi kavu na vile vya Songosongo.

Iwapo kasi ya utafutaji mafuta itaendelea kama sasa katika kipindi cha miaka 2 ijayo Tanzania itaweza kuwa kati ya nchi mbili za Afrika zenye Utajiri mwingi zaidi wa Gesi Asilia. Hivi sasa Nigeria ndio inaongoza kwa kuwa na futi za ujazo trillion 189 (189TCF) ikifuatiwa na Algeria na Angola ambazo zote zina utajiri wa juu kidogo ya 100TCF kwa Algeria na chini ya 100TCF kwa Angola. Msumbiji sasa imeifikia Algeria na kushika nafasi ya pili.

Katika masuala ya Mafuta na Gesi hatua ya kwanza ni kujua kama utajiri huu ambayo kitaalamu inaitwa gas exploration. Shughuli za utafutaji zinapandisha sana thamani ya nchi na eneo la nchi. Kwa mfano hivi sasa kitendo cha Kampuni ya Uingereza ya BG/Ophir na ile ya Norway ya StatOil kupata mafanikio makubwa katika utafutaji wa Gesi asilia kumeongeza thamani ya Pwani ya kusini ya Tanzania katika medani za utafutaji (Exploration Activities).

Hata hivyo kama ilivyogusiwa hapo juu, shughuli za Utafutaji ni shughuli za msimu. Pia huchukua muda mrefu wa kati ya miaka 5 mpaka 10 kati ya kutafuta, kupata na kuanza kuchimba. Hivi sasa ni muda wa pwani ya Afrika Mashariki. Ni lazima kuhakikisha kwamba vitalu vyote vilivyogawiwa hivi sasa vinafanyiwa kazi. Hata hivyo vitalu vingine vyovyote visigawiwe kwanza mpaka hapo matunda ya vitalu vya sasa yaonekane. Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini imependekeza kusimamisha kugawa vitalu vipya. Matokeo ya utafutaji katika vitalu vya sasa yakiwa mazuri kama ilivyo sasa, thamani ya vitalu vipya itapanda sana na nchi itakuwa na nguvu ya majadiliano (strong negotiation position) dhidi ya makampuni makubwa ya mafuta. 

Tufanyaje kuhusu vitalu vilivyogawiwa katika eneo ambalo lina mgogoro kuhusu suala la Muungano? Sio kazi rahisi lakini imefikia wakati tuamue. Kwa kadri nionavyo, Itabidi kuwe na maamuzi ya mpito (interim decisions) na maamuzi ya muda mrefu.

Kwanza, ni lazima kukiri tulipokosea. Hata kama ilikuwa ni sahihi kiutaratibu kuweka suala la mafuta na Gesi katika orodha ya mambo ya Muungano, haikuwa halali Shirika la TPDC lenye mipaka ndani ya Tanzania bara kuingilia ugawaji wa vitalu na kuingia mikataba katika maeneo ambayo ni ya Muungano. Ni Taasisi ya Muungano tu ndio inaweza kushughulikia suala la Muungano na sio vinginevyo.

Ilikuwa ni dharau kubwa sana kwa Waziri wa Nishati ambayo sio Wizara ya Muungano kuingia Mikataba katika eneo la Zanzibar (ambapo kikatiba tumelifanya eneo la Muungano) bila kushauriana na kukubaliana na Waziri wa Nishati wa Zanzibar. Kukiri kosa sio unyonge, ni uungwana. Hata tukifanya vikao milioni moja chini ya Makamu wa Rais, bila kukiri kosa hili tatizo hili na mengine ya aina hii hayataisha.

Pili, ni vema kukubali kwamba shughuli za utafutaji katika vitalu vyenye mgogoro ziendelee kwenye hatua ya utafutaji tu. Kama mafuta au Gesi ikipatikana, uchimbaji usianze mpaka uamuzi wa mwisho kuhusu suala hili uwe umepatikana. Pia ninapendekeza ufumbuzi wa mwisho hapa chini. Kuchelewesha utafutaji ni hasara kwa pande zote za Muungano kutokana na taarifa za kijiolojia zitakazopatikana na hivyo kupandisha thamani ya nchi hizi mbili kijiolojia.

Hata hivyo, utafutaji huu katika eneo lenye mgogoro kati ya pande mbili za Muungano ufanyike baada ya mkataba wa PSA kufanyiwa marekebisho makubwa. Marekebisho hayo ni pamoja na Mkataba kusema wazi kwamba shughuli za uchimbaji zitafanyika iwapo tu makubaliano ya kugawana mapato ya Mafuta na Gesi kati ya Serikali ya Muungano na Serikali ya Zanzibar yamefikiwa. Pia Mkataba uzingatie maendeleo ya sasa ya kusini mwa Tanzania na hivyo mkataba uboreshwe kwa faida ya nchi ikiwemo kutolewa kwa ‘signature bonus’. Hii ni Fedha inayotolewa na Kampuni za utafutaji Mafuta kwa Serikali kabla ya utafutaji kuanza. Kiwango hutokana na majadiliano na kukubaliana. Nchi zenye jiolojia iliyopevuka hutumia njia hii kuongeza mapato ya Serikali.

Mkataba pia useme kinaga ubaga kwamba utasainiwa na Mawaziri wa pande mbili za Muungano na kwamba Kampuni inayofanya utafiti itatoa taarifa zake za Utafiti sawia kwa Mawaziri wote kwa mujibu wa vipengele vya mkataba.

Kwa upande wa maamuzi ya muda mrefu, ushauri wangu ni kwamba; kwa maana ya kuandikwa kwenye Katiba mpya ni kwamba Suala la Mafuta na Gesi Asilia liendelee kuwa suala la Muungano kwenye eneo la usimamizi wa Tasnia na leseni za utafutaji (Upstream Regulatory mechanism). Hili ni eneo linalohitaji usimamizi wa dhati kabisa na kwa pamoja pande mbili za Muungano zinaweza kufanya vizuri zaidi.

Eneo la Uchimbaji na hasa kugawana mapato ya mafuta na Gesi (Profit Oil) lisimamiwe na kila upande wa Muungano kivyake. Biashara ya Mafuta isiwe jambo la Muungano na hivyo kila Upande wa Muungano uwe na Shirika lake la Mafuta na Gesi ambalo litashiriki kama mbia wa Mashirika ya Kimataifa katika uchimbaji, usafirishaji na uuzaji wa Mafuta na Gesi Asilia. Mapato yanayotokana na Mafuta (Profit Oil) na kodi nyingine zote isipokuwa mrahaba (royalty) yawe ni masuala yanayoshughulikiwa na Serikali ya kila upande wa Muungano kwa mujibu wa Sheria ambayo Serikali hizo zimejiwekea.

Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma ilipendekeza Bungeni kwamba kuwepo na Mamlaka ya Mafuta na Gesi Asilia Tanzania (Tanzania Petroleum Authority) ambayo itakuwa ni msimamizi (upstream regulator) kama suala la Muungano. Mrahaba wa Mafuta na Gesi ambao sasa ni asilimia 12 ya Mapato ya Mafuta itakusanywa na Msimamizi huyu na ndio mapato pekee katika tasnia ya Mafuta na Gesi yanapaswa kuwa mapato ya Serikali ya Muungano.

Kamati pia ilipendekeza kuanzishwa kwa Shirika la Mafuta na Gesi (Petroleum Tanzania – PetroTan) ambalo litakuwa mbia kwenye Makampuni ya utafutaji na uchimbaji wa Mafuta na Gesi kwenye Vitalu vya Tanzania bara. Mapato yote ya vitalu vya Tanzania bara na kodi zote isipokuwa Mrahaba zitakwenda kwa Mamlaka za bara tutakazo kuwa tumeamua baada ya Katiba mpya kuanza kazi. Hivi sasa TPDC inafanya kazi hii mpaka Zanzibar jambo ambalo hata kwa akili ya kawaida halipaswi kukubalika.

Aidha, napendekeza kwamba Zanzibar ianzishe Shirika lake la Mafuta sasa. Jambo hili halina haja ya kusubiri vikao vya kero za Muungano kwani ni dhahiri TPDC haina mamlaka,ushawishi na uthubutu kusema uhalali wa kusimamia vitalu vya Mafuta vilivyopo  Zanzibar.

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ipeleke muswada katika Baraza la Wawakilishi kuanzisha Shirika la Mafuta na Gesi la Zanzibar (Petroleum Corporation of Zanzibar – PetroZan) ili liweze kushiriki katika utafutaji na uchimbaji wa Mafuta Zanzibar. Lakini Pia PetroZan ilinde maslahi ya Zanzibar katika tasnia hii kwa kujijengea uwezo wa kusimamia ugawaji bora wa Mapato kutoka katika Mafuta na Gesi Asilia.

Kama Serikali ya Mapinduzi Zanzibar inachelea kuanzishwa kwa Shirika hili, Wawakilishi wa pande zote (CCM na CUF) wapeleke muswada binafsi kuunda Shirika la Mafuta la Wazanzibari. Hawatakuwa wamevunja Katiba ya Muungano kwani hivi sasa hakuna Taasisi yenye mamlaka ya kusimamia Tasnia hii kwa Upande wa Zanzibar.

Wakati haya yote yanafanyika, shughuli za utafutaji Mafuta na Gesi katika vitalu vilivyopo katika eneo la Zanzibar na hasa vitalu namba 9,10,11 na 12 na katika kitalu cha kati ya Pemba na Tanga ziendelee kufuatia marekebisho ya Mkataba wa Utafutaji. Utafutaji wa Mafuta una faida zaidi kwa Nchi hizi mbili kuliko kwa Kampuni za Mafuta kwani uwekezaji wa Kampuni pekee na nchi zitapata taarifa za kijiolojia zitakazosaidia mikataba ya baadaye kuwa bora zaidi.

Wakati nasisitiza kwamba tuendelee na utafutaji katika vitalu tajwa, katika Katiba mpya, utafutaji wa mafuta usimamiwe na Taasisi ya Muungano. Uchimbaji na biashara ya Mafuta ufanywe na kila Serikali ya kila upande wa Muungano. Mafuta kuwa jambo la Muungano halafu kusimamiwa na Shirika la Tanganyika na Wizara ya Upande mmoja ya Muungano ndio chanzo cha mgogoro. Suluhisho sio kuifanya TPDC kuwa Shirika la Muungano, bali kila upande upewe uhuru wa kusimamia uchimbaji, Biashara na mlolongo mzima wa tasnia ya Mafuta (value chain from midstream to downstream) isipokuwa utafutaji (upstream). Hili ndio suluhisho la kudumu ninaloona linafaa. 

Uwazi (declaration):

Zitto Kabwe ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini na mfuatiliaji wa karibu wa Tasnia ya Mafuta na Gesi Asilia akiwa amesomea mfumo wa uchumi wa katika tasnia ya madini na mafuta (fiscal regime in Mineral and Petroleum sector).  Zitto pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma ambayo inasimamia mahesabu na utendaji wa Shirika la TPDC. Makala hii imeandikwa baada ya ziara ya Mafunzo ya Wabunge kutembelea nchi ya Uholanzi kwa ufadhili wa Wizara ya Mambo ya Nje ya nchi hiyo. Katika ziara hiyo Wabunge hao walikutana na Wakuu wa Shirika la Mafuta la Shell ambapo walizungumzia pia suala la vitalu namba 9, 10, 11 na 12.

Muswada wa Marekebisho ya Katiba ujenge Mwafaka wa Kitaifa

with 14 comments

Zitto Kabwe[1], Mb

Kama kuna jambo moja ambalo huunganisha Taifa ni Katiba ya Taifa hilo. Katiba huweka misingi mikuu ya nchi na namna ya kujenga na kuendesha Taifa. Hivyo Katiba inapaswa kuwa ni matokeo ya mwafaka wa kitaifa kwenye masuala yote ya msingi ya nchi husika. Tanzania imekuwa ikiongozwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 kama ilivyofanyiwa marekebisho mara kwa mara. Kabla ya hapo kulikuwa na Katiba ya Uhuru ambayo ilitokana na Mwafaka wa wapigania Uhuru wa nchi yetu, baadaye Katiba ya Jamhuri ya Tangayika na kisha Katiba ya muda ya Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kabla ya kubadili jina na kuitwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Ukiachana na Katiba ya Uhuru, Katiba nyingine zote hazikutokana na mwafaka wa kitaifa bali matakwa ya tabaka la watawala. Katiba ya kudumu ya mwaka 1977 ni zao dhahiri kabisa la utawala wa chama kimoja ambacho kilikuwa na dhamira ya kushika hatamu za uongozi. Kutokana na hali hii haikuchukua muda kwa wasomi mnamo mwaka 1983 kuanza harakati za kuifanyia mabadiliko makubwa. Mabadiliko hayo yalizaa kuwemo kwa Haki za Msingi za Binaadamu katika Katiba katika mabadiliko ya mwaka 1984, miaka saba tu toka kuandikwa kwa Katiba ya kudumu.

Takribani mwaka mzima huu kumekuwa na madai ya kuandikwa kwa Katiba mpya. Madai haya sio mapya kwani huibuka na kusinyaa kila baada ya uchaguzi Mkuu. Itakumbukwa kwamba miaka ya Tisini mwishoni kundi la vyama vya siasa liliunda Kamati ya Mabadiliko ya Katiba (KAMAKA) ili kudai kuandikwa kwa Katiba mpya. Hata hivyo safari hii sauti ya mabadiliko imekuwa ni kubwa sana kiasi cha Serikali kusikia na hivyo kupeleka Bungeni muswada wa Marejeo ya Katiba kwa lengo la kuandika Katiba mpya ya nchi yetu. Muswada huu umeleta kelele nyingi na manung’uniko mengi sana kutoka kwa makundi mbalimbali ya jamii kuanzia vyama vya siasa, viongozi wa dini na Asasi za Kijamii. Baadhi ya Asasi za Kijamii zimeunda Jukwaa la Katiba ili kuweza kuratibu vizuri juhudi za kuandikwa kwa Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Sababu kubwa ya kupingwa kwa muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya mwaka 2011 ni kwamba mchakato umewekwa kwenye Dola mno na hasa kwenye Urais. Rais anateua Tume ya kukusanya maoni, Rais anateua Bunge la Katiba nk. Watu wengi tungependa kuona mchakato unakuwa kwa wananchi zaidi. Serikali imefanya marekebisho kadhaa na kupanua wigo wa mjadala wa Katiba na pia kumhusisha kikamilifu Rais wa Zanzibar katika mchakato.

Baadhi yetu tunaona kama nafasi ya Zanzibar katika mchakato imepewa nguvu kubwa kupita kiasi. Ninadhani Zanzibar inastahili kupata nafasi hii katika mchakato wa Katiba. Jambo ambalo ni vizuri tulitilie maanani ni kwamba Muungano wa Mwaka 1964 ulihusisha nchi mbili huru zenye hadhi sawa mbele ya sheria za kimataifa. Linapokuja suala la kuandika Katiba ya Muungano, pande mbili za Muungano zinakuwa na hadhi sawasawa. Kwamba Zanzibar ishiriki kwenye masuala ya Muungano tu ni hoja inayojadilika iwapo tu Katiba ya Muungano ingetofautisha kinagaubaga taasisi za kimuungano na zisizo. Kwa mfano Sura ya Bunge katika Katiba ni lazima ijadiliwe na pande zote mbili ingawa Bunge wakati mwingine hupitisha miswaada ambayo sio ya masuala ya Muungano. Aina ya Muungano wetu inatulazimisha kufanya hivi tunavyofanya sasa. Mkataba wa Muungano ni lazima uheshimiwe kama ulivyo sasa.

Katiba mpya yaweza kuweka makubaliano mapya lakini muswada wa sasa ni lazima utambue nafasi halali ya Zanzibar kwa mujibu wa Katiba ya sasa na Hati za Muugano. Suala hili ni suala la kisheria na sio suala la idadi ya watu au ukubwa wa eneo la nchi husika. Nchi ya Ushelisheli yenye watu 80,000 ina nafasi sawa na Tanzania yenye watu 42 milioni katika SADC, AU na UNO. Zote zina kura moja tu. Huu ndio ukweli na hatuna budi kukubaliana nao.

Muswada unampa mamlaka Rais wa Tanzania na Rais wa Zanzibar kuteua Tume ya Katiba. Tume hii maRais hawatapata ushauri wa mtu mwingine yeyote  kwa mujibu wa kifungu cha (6) na vifungu vidogo (1), (2) na (3). Wanasiasa wakiwemo Wabunge, Wawakilishi, viongozi wa vyama wa Ngazi za Taifa, Mkoa au Wilaya hawatakuwa na sifa za kuteuliwa.

Inawezekana kabisa waandishi wa muswada walikuwa na mantiki ya kuuondoa mchakato kwenye mikono ya wanasiasa. Nia hii njema haikufikiriwa vizuri hata kidogo. Njia hii haijengi mwafaka. Tume hii sio ya Wataalamu, ni Tume inayopaswa kuwa na sura ya kitaifa. Nafasi ya wanasiasa katika mchakato wa kukusanya maoni ni muhimu sana katika kuhalalisha mchakato wenyewe. Tume lazima ionekane ni Tume ya Taifa na sio Tume ya maRais. Hivyo kipengele hiki cha kuwanyima sifa wanasiasa kinapaswa kufutwa katika muswada. Wabunge na Wawakilishi kwa kuwa ni sehemu ya Bunge la Katiba wasiwemo katika Tume, lakini viongozi wengine wa kisiasa wawe na haki ya kuteuliwa kuwa wajumbe.

Lakini pia Rais ateue Tume kutokana na maoni kutoka katika makundi yenye maslahi ya karibu na Katiba ya nchi na hivi ni vyama vya siasa. Ninapendekeza kwamba katika Wajumbe 30 wa Tume ya kukusanya maoni ya Katiba, 10 watokane na vyama vya siasa vyenye Wabunge kwa uwiano wa CCM 2, CHADEMA 2, CUF 2, NCCR 2, TLP 1 na UDP 1. Kila chama cha siasa chenye Wabunge kupitia kiongozi wake Bungeni kipeleke majina ya watu wanaowapendekeza kuwa katika Tume ya Katiba na kutokana na Mapendekezo hayo Rais atawateua kuwa wajumbe. Masharti mengine ya nusu kutoka kila upande wa Muungano yazingatiwe.

Muswada unapendekeza kuwepo kwa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Tume. Kifungu cha cha 7 kifungu kidogo (1), (2) na (3) kinaweka utaratibu wa kupatikana kwa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Tume. Muswada unasema UTEUZI wa Mwenyekiti na Makamu utazingatia kwamba mmoja atoke uapnde mmoja wa Muungano na mwingine upande wa Pili wa Muungano. Ingawa Muswada hausemi waziwazi lakini ni dhahiri kwamba Mwenyekiti wa Tume atateuliwa na Rais baada ya kushauriana na kukubaliana na Rais wa Zanzibar. Sitaki kujenga hoja kwamba Mwenyekiti na Makamu wachaguliwe na wajumbe wa Tume kutoka miongoni mwao lakini ni dhahiri Mwenyekiti wa Tume anapaswa kuwa mtu mwenye heshima kubwa hapa nchini. Ningependekeza kwamba maRais wateue Wenyeviti wenza badala ya Mwenyekiti na Makamu wake ili kuweka nafasi sawa kwa pande mbili za Muungano. Hapa nchini tunao Watanzania ambao wamefanya kazi iliyotukuka katika nyadhifa mbalimbali na sasa ni wastaafu wasio na nia yeyote ya madaraka ya kisiasa wanaoweza kuongoza vizuri kabisa Tume hii. Ni pendekezo langu kwamba Dkt. Salim Ahmed Salim na Jaji Joseph Sinde Warioba wawe wenyeviti wenza wa Tume ya Katiba. Uzoefu wao katika uongozi na kuijua kwao nchi kutasaidia sana kuhakikisha kwamba mchakato wa kukusanya maoni na kisha kuandika Katiba unakuwa na mafanikio kwa kuzingatia misingi ya Taifa letu.

Muswada unapendekeza kwamba Hadidu rejea za Tume zitolewe na maRais. Kifungu cha nane na muswada kuhusu hadidu rejea nadhani hakina mantiki sana. Madhumuni ya muswada yanasema pamoja na mambo mengine muswada unaweka masharti kuhusu Hadidu rejea za Tume. Wakati huo huo muswada unasema Hadidu rejea zitakuwa ni hati ya kisheria itakayozingatiwa na Tume katika kazi zake.

Mantiki ni kwamba Hadidu rejea zinapaswa kuwa sehemu ya Muswada kama ‘schedule’ ili kuzipa nguvu ya kisheria badala ya tangazo katika gazeti la Serikali. Hadidu rejea zikiwa ni sehemu ya Muswada zitajadiliwa na Bunge na kupitishwa hivyo kuwa ni jambo ambalo limefikiwa kwa mwafaka wa wawakilishi wa wananchi.

Muswada unataka uamuzi wa kura ya maoni kuhusu Katiba uwe ni kukubaliwa na nusu ya Watanzania katika kila upande wa Muungano. Nadhani hapa tunacheza na Katiba ya nchi. Katiba ya nchi inapaswa kukubaliwa na theluthi mbili ya wapiga kura wa pande zote za Muungano yaani kila upande theluthi mbili. Hii itaipa Katiba ‘legitimacy’ na hivyo kuheshimiwa na wananchi na watawala. Kuna woga gani uliopo kutaka katika ikubalike na nusu ya wapiga kura? Mifano ya nchi nyingi duniani Katiba inapaswa kukubaliwa na theluthi mbili ya wapiga kura. Hata jirani zetu wa Kenya ilikuwa hivyo na hata kura ya maoni kuhusu mwafaka huko Zanzibar ilikuwa hivyo. Kwa kuwa Katiba ni chombo cha mwafaka wa kitaifa, muswada utamke kwamba Katiba mpya itakuwa imepita iwapo theluthi mbili ya wapiga kura watapiga kura ya ndio.

 mwisho


[1] Zitto Kabwe ni Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kaskazini na Naibu Katibu Mkuu CHADEMA. Maoni haya ni maoni binafsi ya Zitto na kwa vyovyote vile hayawakilishi msimamo rasmi wa CHADEMA au Kambi ya Upinzani Bungeni.

Written by zittokabwe

November 7, 2011 at 11:52 AM