Zitto na Demokrasia

Zitto na Demokrasia

Posts Tagged ‘Mafuta na Gesi Asilia

Mtwara : Serikali inavunja nchi kwa kutosikiliza Wananchi

with 13 comments

Mtwara : Serikali inavunja nchi kwa kutosikiliza Wananchi

Kwa wiki ya tatu mfululizo kumekuwa na malumbano kuhusiana na suala la ujenzi wa Bomba la gesi kutoka Mtwara mpaka Dar es Salaam. Kumekuwa na madai yenye nguvu ya hoja kutoka kwa wananchi wa Mtwara dhidi ya porojo kutoka kwa viongozi wenye dhamana ya kujibu madai haya ya watu wa Mtwara. Watu wa Mtwara kwa umoja wao na kwa kuungwa mkono na viongozi wa dini zote wamekuwa wakitaka Serikali ifikirie upya suala la mradi wa ujenzi wa Bomba la gesi na badala yake kujenga mitambo ya kufua umeme mkoani Mtwara na kusafirisha umeme huo kwenda maeneo mengine ya nchi. Kwenye moja ya maandishi yangu (Serikali iwasikilize watu wa Mtwara) nimeshauri kuwa Taifa liwe na gridi nyingine ya Taifa ambayo itatokana na Gesi tu na ianzie Mtwara.

Ikumbukwe kwamba katiba ya nchi, ibara ya 9 katika mabano J inataka mamlaka ya dola na vyombo vyake vyote kuhakikisha ya kwamba shughuli zote za kiuchumi zinaendeshwa kwa namna ya kwamba pasiwe mrundikano wa utajiri au shughuli za uzalishaji kwa watu wa chache. Katiba inaendela kwa kuelekeza kwamba uchumi wa nchi upangwe katika uwiano sawia (9, d). Watu wa Mtwara wanatekeleza matakwa haya ya katiba kwa kukataa mrundikano wa shughuli za kiuchumi wa nchi na utajiri wa nchi kua kwenye mikoa michache na hasa mkoa wa Dar-Es-Saalam.

Serikali imekuwa ikitoa majibu ya porojo na kuwatusi watu wa Mtwara na kama ilivyozoeleka Rais Jakaya Kikwete na Mawaziri wake wamekuwa wakisema suala la Mtwara linatumika na wanasiasa kujitafutia umaarufu. Inasikitisha sana kuona Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwaambia mabalozi wa nchi za kigeni waliopo hapa nchini kuwa yanayoendelea mkoani Mtwara yanachochewa na Wanasiasa tuliosimama na wananchi wanaodai haki ya kufaidi utajiri wa nchi yetu. Rais Kikwete na Mawaziri wake wameshindwa kabisa kuonyesha uongozi katika suala hili na hatimaye kuhatarisha umoja wa kitaifa.

Kwa udhaifu wa serikali na tabia ya kutafuta mchawi badala ya kutatua tatizo la msingi, wananchi wameendelea kukutana na hata wengine sasa kuanza kusambaza ujumbe wa kukata kipande cha nchi na kuanzisha Jamhuri ya Kusini. Nimeona kwenye mabango ya mkutano wa hadhara uliofanyika 19/1/2013 wananchi wakibeba mabango yanayoaishiria kuchoka kuwa sehemu ya Tanzania na kuanzisha Jamhuri ya Makonde kuanzia jiwe la Mzungu wilayani Kilwa mpaka mto Ruvuma. Haya yanatoka na kiburi cha Serikali kujishusha na kuwasikiliza wananchi wanao dai haki yao ya kikatiba.

Ni Serikali iliyokosa uhalali wa kutawala inayoweza kudharau hisia hizi za wananchi. Serikali ielewe kwamba kamwe haitaweza kulinda kila nchi ya bomba hili iwapo italijenga kwa nguvu. Badala ya kuzungumza na vyombo vya habari Serikali ifanye mazungumzo na wananchi wa Mtwara na kukubaliana na matakwa yao. Kitendo cha Serikali kung’ang’ania msimamo wake dhidi ya watu wa mtwara ni kitendo kinacho weza kuipasua nchi na hivyo kwenda kinyume na masharti ya katiba ibara ya 28 ambayo inasema: “kila raia ana wajibu wa kulinda uhuru wa nchi, uhuru mamlaka na umoja wa taifa.”ibara ya 28, 1.

Inawezekana Serikali inaogopa kuvunja makubaliano na Wachina ya mkopo wa dola za kimarekani 1.2 bilioni ambao imeuingia bila hata kushirikisha Bunge. Inawezekana Serikali na hasa watendaji wa Serikali waliojadili mkopo huu wameshapata chao na hivyo kuogopa kusikiliza madai halali ya wananchi. Lakini yote hayo hayawezi kuwa zaidi ya Umoja wa nchi yetu. Hatuwezi kukubali nchi yetu ipasuke vipande vipande kwa sababu tu ya kulinda mkataba wa bilioni 1.2 tuliokopa China, ambayo serikali inang’ang’ania.

Tunafahamu kwamba ubalozi wa China umeandika barua serikalini kuwaondoa raia wa China waliopo Mtwara kwa hofu ya maisha yao. Serikali inaficha ukweli huu kama ilivyoficha ukweli kwamba Naibu Waziri wa Nishati na Madini bwana George Simbachawene alifukuzwa na wananchi wa Mtwara alipokwenda hivi majuzi. Serikali itaficha ukweli mpaka lini? Lazima tupate majawabu.

Kwanza Serikali iweke wazi mkataba wa ujenzi wa Bomba hili. Kamati ya Bunge ya POAC ilipokuwa inapitia mahesabu ya TPDC iliomba mkataba na kwa mshangao mkubwa wabunge wakaambiwa Mkataba haupo TPDC bali upo Wizarani. Kwa nini Mkataba huu wa matrilioni ya Fedha unafichwa? Mkataba huu ulisainiwa pamoja mikataba mingine 2, mmoja wa kujenga nyumba za wanajeshi wa thamani ya dola za kimarekani 400 milioni na mwingine wa mawasiliano jeshini wa dola za kimarekani 110 milioni, na mikataba yote mitatu imesainiwa kimya kimya bila kushirikisha wananchi kupitia Bunge. Lazima mikataba yote hii iwekwe wazi.

Pili, Mkataba huu uchunguzwe kama unalingana na thamani ya fedha maana kwa utafiti wa awali inaonyesha kuwa bei ya ujenzi wa bomba imepandishwa maradufu. Wastan wa kujenga bomba la gesi duniani ni dola za kimarekani 1.2 milioni kwa maili moja. Mradi huu wa Tanzania utagharimu dola za kimarekani 2.2 milioni kwa kilomita moja (maili 1 ni sawa na kilomita 1.6).

Tatu, Serikali ibadilishe Mkataba huu kuwa wa mkopo wa kujenga Mitambo ya kufua umeme Mtwara na ujenzi wa Msongo wa Umeme kama gridi ya pili ya Taifa. Kwa sasa Tanzania ina gridi moja ambayo inabebwa na bwawa la Mtera linalo tegemea mto Ruaha ambao hivi sasa unakauka miezi 5 katika miezi 12 ya mwaka. Ni dhahiri kwamba kwa usalama wa Taifa na hata kwa gharama Nchi itafaidika zaidi kwa kujenga gridi nyingine kutokea Mtwara badala ya kusafirisha gesi kuja Dar-Es-Salaam.

Serikali haitashinda vita hii kwa kuzusha kwamba ama wanasiasa wanaopinga wanatumika na makampuni mengine au kwa mataifa ya magharibi kutaka kuvuruga nchi. Serikali ijitazame yenyewe. Bila kufanya hayo tunayo pendekeza hapo juu, wananchi wataendelea kupigania hako yao. Hii ni vita ya uwajibikaji. Wananchi wanataka kufaidika na rasilimali za nchi yao. Kwa vyovyote vile upande wa wananchi utashinda. Vita ya uwajibikaji kwenye rasilimali za nchi sio ya vyama vya siasa, ni vita ya wananchi. Chama cha siasa kitakachokwenda kinyume na matakwa ya wananchi, kinajichimbia kaburi.

 

 

Mchango wangu Bungeni-Hotuba ya Waziri Mkuu: Haki za Uraia, Mafuta/Gesi Asilia na Uwajibikaji

with 18 comments

MHE. ZITTO Z. KABWE:

Haki za Uraia, Mafuta/Gesi Asilia na Uwajibikaji

Unyanyasi wa Watu wa Kigoma

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia Hotuba hii ya Waziri Mkuu. Jana Mheshimiwa Waziri amekuja kuomba Bunge limuidhinishie jumla ya shilingi trilioni 3.8 kwa ajili ya Ofisi yake na taasisi zote zilizo chini ya Ofisi yake pamoja na takribani shilingi bilioni 113 kwa ajili ya Bunge. Fedha zote hizi takribani shillingi trilioni 3.2 zinakwenda Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla hatujaweza kumuidhinishia Mheshimiwa Waziri Mkuu fedha hizi na yeye kama Mkuu wa Shughuli za Serikali, msimamizi wa kazi za Serikali za kila siku na ambaye anaangalia utendaji wa takribani Mawaziri, wote ni vizuri aweze kutoa majibu kwa baadhi ya masuala ambayo mengine ameyaainisha kwenye hotuba yake, lakini mengine hakuyaainisha katika hotuba yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza na Kigoma. Mheshimiwa Waziri Mkuu katika ukurasa wa 51 wa Hotuba yake amezungumzia masuala ya ulinzi na usalama lakini hakugusia kabisa operesheni ambazo zinaendelea hivi sasa katika Mkoa wa Kigoma nadhani na Mkoa wa Kagera kuhusiana na masuala ya wahamiaji haramu. Hivi tunavyozungumza ni kwamba mamia ya watu wa Kigoma wameonyeshwa kwamba siyo raia wa Tanzania. Utaratibu huu umekuwa ukiendelea mwaka hadi mwaka. Napenda Mheshimiwa Waziri Mkuu akumbuke historia baada ya Vita vya Kwanza vya Dunia kati ya mwaka 1918 na mwaka 1924 Kigoma haikuwa sehemu ya Tanganyika. Kigoma ilikuwa inatawala kama inavyotawaliwa tofauti sasa hivi Burundi kama inavyotawaliwa sasa tofauti Rwanda. Kwa muda mrefu sana Mkoa wa Kigoma umeachwa nyuma katika kila kitu eneo la maendeleo.

Mimi nimeona lami ya kwanza ya highway mwaka 2008. Miaka zaidi ya 40 baada ya uhuru. Leo hii watu wa Kigoma wa maeneo ya Kusini mwa Kigoma wa maeneo ya Kaskazini mwa Kigoma wanasombwa kwenye maboti, wanasomwa kwenye magari wakiambiwa kwamba siyo raia wa Tanzania. Hatuwaoni Wamakonde wakiambiwa kwamba siyo raia wa Tanzania na wanapakana na Msumbiji. Hatuwaoni Wamasai wanaambiwa siyo raia wa Tanzania na wanapakana na Kenya. Hatuwaoni Wachaga wanaambiwa siyo raia wa Tanzania wanapakana na Kenya. Hatuwaoni Wanyakyusa wanaambiwa siyo raia wa Tanzania wanapakana na Zambia na vile vile wanapakana na Malawi.

Kwa nini suala hili liwe ni kwa watu wa Kigoma na watu wa Katavi peke yake? Kwa nini tunatumia fedha za nchi, polisi wa nchi kwenda kusumbua watu wa Kigoma. Nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu operesheni inaendelea sasa hivi katika Mkoa wa Kigoma kuwanyanyasa Raia wa Kigoma waonekane ni Raia wa Tanzania wa daraja B ikome mara moja na viongozi wa Kisiasa, Wabunge wote  wa Mkoa wa Kigoma na Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa tukae tuweze kuangalia kwa sababu kuna uonevu wa hali ya juu sana katika operesheni ambayo inaendelea hivi sasa.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba niyaseme hayo vizuri na ninarejea kwamba tumefundishwa na wazee wetu kwamba sisi kati ya mwaka 1918 na mwaka 1924 hatukuwa sehemu ya Tanganyika iliyokuwa inatawaliwa na Mwingereza. Ninaomba nirejee sisi ni watu wa Kigoma kwanza kabla hatujawa wa Tanganyika, kabla hatujawa Watanzania. Ninaomba nilisisitize hili na watu wa Kigoma wananisikia kwa sababu tumenyanyaswa sana. Ninaomba masuala ya uraia yaangaliwe kwa karibu sana. Huu ni ujumbe ambao nimepewa na watu wa Kigoma nimeombwa niueleze na naomba Ofisi ya Waziri Mkuu, Mkuu wa Kigoma yupo hapa, Wakuu wa Wilaya, Kamanda Mkuu wa Mkoa wa Polisi wa Mkoa wa Kigoma na IGP waweze kuliangalia jambo hili kuweza kuhakikisha kwamba tunawalinda raia wa Kigoma.

Wenye Mabilioni Uswisi(Switzerland)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, Mheshimiwa Waziri Mkuu kumekuwa na taarifa ambazo zimeandikwa katika vyombo vya habari toka wiki iliyopita. Lilianza Gazeti la The East African baadaye wakaja Gazeti la The Citizen na leo nimesikia kwamba Gazeti la Mwananchi limezungumza kwamba kuna Watanzania 6 wana fedha katika akaunti kule Uswisi zaidi ya shilingi bilioni 303. India walipopata taarifa hizi kutoka Benki ya Uswisi waliwataja majina watu wote wana siasa na wafanyabiashara wenye fedha nje na fedh zile zikachunguzwa zile ambazo zimepatikana kwa haramu zikarejeshwa India. Nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu uagize TAKUKURU na vyombo vyote vya Ulinzi na Usalama kwanza tutambue ni Watanzania gani hawa na fedha hizi zimepatikana kwa njia zipi na zile ambazo zimepatikana kwa njia ya wizi na ufisadi zirejeshwe nchini mara moja. Kwa sababu hatujaanza kunyonya utajiri huu wa gesi tayari kuna watu ambao wameshaanza kutajirika nao.

Tutakapoanza kunyonya hali itakuwaje? Kwa hiyo, nilikuwa naomba suala hili Serikali ilichukulie kwa uzito mkubwa ili itume salaam kwa mtu yeyote ambaye anatarajia kwamba atafaidika na utajiri wa rasilimali ya nchi kama gesi na madini na kadhalika ajue kwamba kokote atakapoficha fedha zake tutazifuata na zitarudi katika nchi hii. Nilikuwa naomba Waziri Mkuu aweze kuliangalia jambo hili kwa ukaribu sana.

Zuia Makampuni ya Kigeni kwenye Ulinzi

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu hivi sasa Kiongozi wa Upinzania amezungumza jana kuna meli ziko Pwani ya Mkoa wa Pwani, Lindi na Mtwara zinatafuta mafuta. Mheshimiwa Waziri Mkuu hakuna kampuni hata moja ya mafuta inayonunua hata mchicha kutoka Tanzania. Meli zote ambazo ziko Bandari Mtwara zinakwenda kupeleka huduma kwenye maeneo ambayo yanatafuta mafuta yanapata mchele, nyanya, vitunguu, mchicha, mafuta ya kula na kadhalika kutokea Kenya kwa sababu hatujaweka utaratibu wa kufanya nchi yetu iweze kufaidika na utaraji huu mwanzoni. Kwa sababu hatua hizi za mwanzoni hakuna kodi ambayo tunapata kwa sababu mafuta bado yanatafutwa.

Hatua hizi za mwanzoni tunatakiwa tufaidike na fedha inayokuja, watu waweze kutumia fedha za kutoka ndani. Lakini hali ilivyo hivi sasa ni kwamba makampuni ya mafuta yanatumia zaidi ya dola milioni 161 kwa ajili ya shughuli za ulinzi na makampuni yanayolinda, ni makampuni ya nje. Yanabeba silaha kubwa kubwa, siku yakiamua kutugeuka na Navy yetu ilivyo tutapata shida. Nilikuwa naomba tutenge resources za kutosha na hata kama hatujaziweka kwenye bajeti sasa hivi, tuangalie, tuimarishe Navy na tupige marufuku, tuandike sheria kabisa kwamba itakuwa ni marufuku kwa raia yeyote wa kigeni kubeba silaha zozote kubwa ili kuweza kuhakikisha kwamba ulinzi ama unafanywa na watu wa ndani au unafanywa na Navy yetu tuweze kulinda mipaka yetu vizuri.

Utafutaji Mafuta Zanzibar Uendelee

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili kuna suala ambalo halijaisha na Kiongozi wa Upinzani Bungeni jana amelizungumzia la mafuta na gesi katika masuala ya muungano. Nilikuwa naomba jambo hili tulimalize kwa haraka. tulimalize kwa haraka na mimi sioni ubaya kwa kweli, sioni ubaya hata kidogo kama tukiamua kwamba shughuli zote commercial not upstream, sio masuala ya regulation, sio masuala ya vibali, sio masuala ya kutoa leseni, masuala yote commercial yanayohusiana na mafuta na gesi, kila upande wa muungano ushughulike na masuala yake.

Hakuna sababu ya kunga’gania jambo hili kama sisi tuna dhahabu, tuna tanzanite, tuna madini hayapo sehemu ya muungano, kwa nini mafuta na gesi yawe sehemu ya muungano? Hili ni jambo ambalo tulimalize, liishe tuimalize hii kero, vikao na vikao havitasaidia, tuimalize hii kero, tu-move forward watu wa Zanzibar waanze utaratibu wao wa kufanya utafutaji wao, waangalie kama watayapata hayo mafuta au hawatayapata, sisi tayari huku Bara tumeshapata, tuna matrilioni ya gesi, basin a wenyewe tuwaache waendelee na utaratibu wao. Hakuna sababu ya kuchelewesha jambo hili tuweze kulimaliza mapema.

TZS 40 Bilioni kwa Kiwira

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni suala la Kiwira na baadae nitakuwa na mazungumzo na baadhi ya Mawaziri kuhusiana na suala hili tuliangalie kwa makini. Tumetenga shilingi bilioni 40 kwenye fedha ya maendeleo Wizara ya Nishati na Madini kwa ajili ya nini? Kuna fedha ambayo tunaenda kuwalipa watu ambao wameuharibu mgodi. Kwa nini tulipe watu ambao wameuharibu mgodi?

Lakini tunaenda kulipa bilioni 40 sio kwa Kiwira nzima..

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

******

Related Story in THE Citizen(Wednesday, 27 June 2012):  Zitto wants Swiss bank accounts investigated probed

Mafuta kuwa suala la Muungano tulikosea

with 17 comments

  • Kila upande wa Muungano uchimbe Mafuta na Gesi Asili yake na Mapato yawe ya Serikali ya upande husika.
  • Shughuli za Utafutaji kwenye vitalu vyenye mgogoro ziendelee mara moja
  • Zanzibar ianzishe Shirika lake la Mafuta (PetroZan)
  • Katiba mpya itofautishe utafutaji (upstream) na Biashara (uchimbaji, midstream na downstream)

Moja ya suala linalosubiriwa kwa hamu kubwa katika mjadala na hatimaye uandishi wa Katiba mpya ni suala la Mafuta na Gesi Asilia kuwa jambo la Muungano au liondolewe katika orodha ya mambo ya Muungano. Suala hili limezusha mjadala mkubwa sana mara kwa mara nchini Tanzania kiasi cha lenyewe kuwa ni hoja ya wale wasiotaka tuwe na Dola ya Jamhuri ya Muungano Tanzania.

Wakati Muungano unaanzishwa mwaka 1964 Mafuta na Gesi hayakuwa masuala ya Muungano. Nimeangalia katika Hati ya Muungano ambayo ilikuwa ni sehemu ya Katiba ya Muda ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka 1965, suala hili halikuwamo katika orodha ya mambo Kumi na Moja ya Muungano. Nyaraka nilizoziona zinaonyesha kwamba suala la Mafuta na Gesi Asilia liliongezwa katika orodha ya Mambo ya Muungano mwaka 1968. Kuna watu wanahoji kihalali kabisa kwamba nyongeza ya jambo hili ilifanywa bila kufuata taratibu na hivyo kufanywa kinyemela na kuna wengine wanasema jambo hili lilifuata taratibu zote za kisheria ikiwemo kupigiwa kura na Bunge la Muungano na kuungwa mkono na theluthi mbili ya Wabunge kutoka pande zote za Muungano.

Katika moja ya vikao vya Bunge katika Bunge la Tisa, aliyekuwa Naibu wa Waziri wa Nishati na Madini Ndugu Adam Malima alileta kumbukumbu za mjadala Bungeni (Hansard) za mjadala wa suala la Mafuta na Gesi ili kuthibitisha kwamba jambo hili halikuuingizwa kwenye Katiba kinyemela.

Wakati umefika kwa Watafiti wa Masuala ya Muungano wakapekua nyaraka hizi na kutwambia ukweli ulio ukweli mtupu wa namna suala la Mafuta na Gesi lilivyoingizwa katika orodha ya mambo ya Muungano. Hata hivyo, jambo hili sasa ni jambo la Muungano kwa mujibu wa Katiba na ni dhahiri kuwa WaTanzania wa Zanzibar hawafurahiswhi nalo na hivyo kuazimia kupitia Azimio la Baraza la Wawakilishi kwamba jambo hili liondolewe kwenye orodha ya masuala ya Muungano. Kwa vyovote vile Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inapaswa kutoa uamuzi wa mwisho utakaomaliza mjadala huu.

Jambo la kusikitisha ni kwamba licha ya Bunge la Muungano kuamua kuongeza suala la Mafuta na Gesi asilia katika masuala ya Muungano, mwaka mmoja baada ya uamuzi huo likaundwa Shirika la Maendeleo ya Mafuta Tanzania (TPDC) kwa amri ya Rais wa Jamhuri ya Muungano (establishment order). Shirika hili halikuanzishwa kwa Sheria ya Bunge au kwa Sheria ya Makampuni kama yalivyo Mashirika mengi ya Umma hapa nchini bali kwa amri ya Rais ya mwaka 1960. Katika amri hii ya Rais, Shirika la TPDC halikupewa ‘mandate’ ya kimuungano. Shirika hili mipaka yake ilianishwa kuwa ni Tanzania bara peke yake. Hivyo suala la Muungano likawekewa Shirika la Tanganyika kulisimamia!

Kama ilikuwa ni bahati mbaya au makusudi au kupitiwa kwa viongozi wetu wa wakati huo ni vigumu kujua lakini huu ni mkanganyiko mkubwa ambao ulipaswa kurekebishwa mapema sana.

Shirika la TPDC limekuwa likifanya kazi ya kusimamia Sekta ya Mafuta na Gesi ikiwemo kutoa vibali vya kutafuta mafuta, kuingia mikataba na Makampuni ya kimataifa na kuisimamia mikataba hiyo. Miongoni mwa mikataba hiyo ni kwenye maeneo ambayo kama isingekuwa Muungano yangekuwa ni Maeneo ya Jamhuri ya Watu wa Zanzibar. Mbaya zaidi Mikataba yote ya utafutaji na uchimbaji Mafuta inafanywa inaingiwa na Waziri wa Nishati na Madini Wizara ambayo sio ya Muungano. Hakuna hata eneo moja ambalo taratibu zimewekwa kwamba pale ambapo eneo hilo ni eneo lilikuwa chini ya himaya ya Jamhuri ya Watu wa Zanzibar basi mikataba isainiwe na Mawaziri wawili wa sekta hiyo kutoka kila upande wa Muungano.

Ni dhahiri kwamba kama ni kusahau hapa kulikuwa na kusahau kukubwa ambako hakustahmiliki kwa mtu yeyote mwenye upeo achilia mbali mwananchi wa kawaida wa Zanzibar ambaye anaona anaonewa na kugandamizwa na Bara.

Mnamo miaka ya mwanzo ya 2000, Shirika la TPDC liliingia mikataba ya Vitalu kadhaa vya Mafuta miongoni vya vitalu hivyo ni vitalu nambari 9, 10, 11 na 12 mashariki ya visiwa vya Pemba na Unguja. Vile vile Shirika na Wizara ya Nishati waliingia mkataba mwingine katika Kitalu kilichopo kati ya Pemba na Tanga (mahala ambapo kumekuwa na dalili za wazi za kuwapo Mafuta kutokana na kuonekana kwa ‘Oil sips’ mara kwa mara.

Vitalu 9, 10, 11 na 12 vilipewa kampuni ya Shell ya Uholanzi na kitalu cha kati ya Tanga na Pemba walipewa Kampuni ya Antrim ya Canada ambayo baadaye waliuza sehemu ya Kampuni yao kwa Kampuni ya RAK Gas kutoka Ras Al Khaimah huko United Aarab Emirates. Kwa kuwa Vitalu hivi vipo katika eneo la iliyokuwa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar kabla ya Muungano, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ilikataa shughuli zozote kufanyika mpaka suala la Mafuta na Gesi kuondolewa katika orodha ya Mambo ya Muungano lipatiwe ufumbuzi.

Uamuzi huu wa Serikali ya Zanzibar ni uamuzi ambao ungechukuliwa na Serikali yeyote ile yenye mapenzi ya dhati na watu wake. Uamuzi huu ulileta mjadala mpana sana katika masuala ya Muungano na ambao hawana taarifa waliubeza sana. Hata hivyo suala hili likafanywa ajenda katika vikao vya masuala ya Muungano vinavyoitwa Vikao vya Kero za Muungano. Miaka kumi suala hili linajadiliwa na Maamuzi hayafanyiki! Hivi sasa kila suala lenye kuangukia kwenye Katiba husukumwa huko na hivyo kutoa ahueni kwa wanaogopa kufanya maamuzi.

Katika medani za uchumi kila suala lina muda wake. Masuala ya utafutaji wa Mafuta ni masuala yanayoongozwa na msimu na kuendelea kuchelewa kufanya maamuzi juu ya suala hili kunalitia hasara Taifa, Hasara ya Mabilioni ya Fedha na hasara kubwa zaidi ya kufahamu utajiri uliojificha chini ya Maji ya Bahari inayozunguka Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Hivi sasa Pwani ya Afrika Mashariki inarindima (trending) katika utafutaji wa Mafuta na Gesi asilia. Huko Msumbiji Makampuni mbalimbali yamegundua Gesi asilia nyingi inayofikia zaidi ya futi za ujazo trillion 107 (107TCF) kwa makadirio ya chini. Hapa Tanzania utajiri wa Gesi asilia uliogunduliwa hadi hivi sasa na kutangazwa umefikia futi za ujazo trillion 20 (20TCF) ambazo ni sawa na utajiri wa thamani ya dola za kimarekani trillion 6. Makadirio yanakisiwa kuwa Tanzania kuna  futi za ujazo trillioni 85 (85TCF) za Gesi Asilia katika eneo la Kusini kuanzia vitalu namba 1 mpaka namba 5 ikiwemo vitalu vya nchi kavu na vile vya Songosongo.

Iwapo kasi ya utafutaji mafuta itaendelea kama sasa katika kipindi cha miaka 2 ijayo Tanzania itaweza kuwa kati ya nchi mbili za Afrika zenye Utajiri mwingi zaidi wa Gesi Asilia. Hivi sasa Nigeria ndio inaongoza kwa kuwa na futi za ujazo trillion 189 (189TCF) ikifuatiwa na Algeria na Angola ambazo zote zina utajiri wa juu kidogo ya 100TCF kwa Algeria na chini ya 100TCF kwa Angola. Msumbiji sasa imeifikia Algeria na kushika nafasi ya pili.

Katika masuala ya Mafuta na Gesi hatua ya kwanza ni kujua kama utajiri huu ambayo kitaalamu inaitwa gas exploration. Shughuli za utafutaji zinapandisha sana thamani ya nchi na eneo la nchi. Kwa mfano hivi sasa kitendo cha Kampuni ya Uingereza ya BG/Ophir na ile ya Norway ya StatOil kupata mafanikio makubwa katika utafutaji wa Gesi asilia kumeongeza thamani ya Pwani ya kusini ya Tanzania katika medani za utafutaji (Exploration Activities).

Hata hivyo kama ilivyogusiwa hapo juu, shughuli za Utafutaji ni shughuli za msimu. Pia huchukua muda mrefu wa kati ya miaka 5 mpaka 10 kati ya kutafuta, kupata na kuanza kuchimba. Hivi sasa ni muda wa pwani ya Afrika Mashariki. Ni lazima kuhakikisha kwamba vitalu vyote vilivyogawiwa hivi sasa vinafanyiwa kazi. Hata hivyo vitalu vingine vyovyote visigawiwe kwanza mpaka hapo matunda ya vitalu vya sasa yaonekane. Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini imependekeza kusimamisha kugawa vitalu vipya. Matokeo ya utafutaji katika vitalu vya sasa yakiwa mazuri kama ilivyo sasa, thamani ya vitalu vipya itapanda sana na nchi itakuwa na nguvu ya majadiliano (strong negotiation position) dhidi ya makampuni makubwa ya mafuta. 

Tufanyaje kuhusu vitalu vilivyogawiwa katika eneo ambalo lina mgogoro kuhusu suala la Muungano? Sio kazi rahisi lakini imefikia wakati tuamue. Kwa kadri nionavyo, Itabidi kuwe na maamuzi ya mpito (interim decisions) na maamuzi ya muda mrefu.

Kwanza, ni lazima kukiri tulipokosea. Hata kama ilikuwa ni sahihi kiutaratibu kuweka suala la mafuta na Gesi katika orodha ya mambo ya Muungano, haikuwa halali Shirika la TPDC lenye mipaka ndani ya Tanzania bara kuingilia ugawaji wa vitalu na kuingia mikataba katika maeneo ambayo ni ya Muungano. Ni Taasisi ya Muungano tu ndio inaweza kushughulikia suala la Muungano na sio vinginevyo.

Ilikuwa ni dharau kubwa sana kwa Waziri wa Nishati ambayo sio Wizara ya Muungano kuingia Mikataba katika eneo la Zanzibar (ambapo kikatiba tumelifanya eneo la Muungano) bila kushauriana na kukubaliana na Waziri wa Nishati wa Zanzibar. Kukiri kosa sio unyonge, ni uungwana. Hata tukifanya vikao milioni moja chini ya Makamu wa Rais, bila kukiri kosa hili tatizo hili na mengine ya aina hii hayataisha.

Pili, ni vema kukubali kwamba shughuli za utafutaji katika vitalu vyenye mgogoro ziendelee kwenye hatua ya utafutaji tu. Kama mafuta au Gesi ikipatikana, uchimbaji usianze mpaka uamuzi wa mwisho kuhusu suala hili uwe umepatikana. Pia ninapendekeza ufumbuzi wa mwisho hapa chini. Kuchelewesha utafutaji ni hasara kwa pande zote za Muungano kutokana na taarifa za kijiolojia zitakazopatikana na hivyo kupandisha thamani ya nchi hizi mbili kijiolojia.

Hata hivyo, utafutaji huu katika eneo lenye mgogoro kati ya pande mbili za Muungano ufanyike baada ya mkataba wa PSA kufanyiwa marekebisho makubwa. Marekebisho hayo ni pamoja na Mkataba kusema wazi kwamba shughuli za uchimbaji zitafanyika iwapo tu makubaliano ya kugawana mapato ya Mafuta na Gesi kati ya Serikali ya Muungano na Serikali ya Zanzibar yamefikiwa. Pia Mkataba uzingatie maendeleo ya sasa ya kusini mwa Tanzania na hivyo mkataba uboreshwe kwa faida ya nchi ikiwemo kutolewa kwa ‘signature bonus’. Hii ni Fedha inayotolewa na Kampuni za utafutaji Mafuta kwa Serikali kabla ya utafutaji kuanza. Kiwango hutokana na majadiliano na kukubaliana. Nchi zenye jiolojia iliyopevuka hutumia njia hii kuongeza mapato ya Serikali.

Mkataba pia useme kinaga ubaga kwamba utasainiwa na Mawaziri wa pande mbili za Muungano na kwamba Kampuni inayofanya utafiti itatoa taarifa zake za Utafiti sawia kwa Mawaziri wote kwa mujibu wa vipengele vya mkataba.

Kwa upande wa maamuzi ya muda mrefu, ushauri wangu ni kwamba; kwa maana ya kuandikwa kwenye Katiba mpya ni kwamba Suala la Mafuta na Gesi Asilia liendelee kuwa suala la Muungano kwenye eneo la usimamizi wa Tasnia na leseni za utafutaji (Upstream Regulatory mechanism). Hili ni eneo linalohitaji usimamizi wa dhati kabisa na kwa pamoja pande mbili za Muungano zinaweza kufanya vizuri zaidi.

Eneo la Uchimbaji na hasa kugawana mapato ya mafuta na Gesi (Profit Oil) lisimamiwe na kila upande wa Muungano kivyake. Biashara ya Mafuta isiwe jambo la Muungano na hivyo kila Upande wa Muungano uwe na Shirika lake la Mafuta na Gesi ambalo litashiriki kama mbia wa Mashirika ya Kimataifa katika uchimbaji, usafirishaji na uuzaji wa Mafuta na Gesi Asilia. Mapato yanayotokana na Mafuta (Profit Oil) na kodi nyingine zote isipokuwa mrahaba (royalty) yawe ni masuala yanayoshughulikiwa na Serikali ya kila upande wa Muungano kwa mujibu wa Sheria ambayo Serikali hizo zimejiwekea.

Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma ilipendekeza Bungeni kwamba kuwepo na Mamlaka ya Mafuta na Gesi Asilia Tanzania (Tanzania Petroleum Authority) ambayo itakuwa ni msimamizi (upstream regulator) kama suala la Muungano. Mrahaba wa Mafuta na Gesi ambao sasa ni asilimia 12 ya Mapato ya Mafuta itakusanywa na Msimamizi huyu na ndio mapato pekee katika tasnia ya Mafuta na Gesi yanapaswa kuwa mapato ya Serikali ya Muungano.

Kamati pia ilipendekeza kuanzishwa kwa Shirika la Mafuta na Gesi (Petroleum Tanzania – PetroTan) ambalo litakuwa mbia kwenye Makampuni ya utafutaji na uchimbaji wa Mafuta na Gesi kwenye Vitalu vya Tanzania bara. Mapato yote ya vitalu vya Tanzania bara na kodi zote isipokuwa Mrahaba zitakwenda kwa Mamlaka za bara tutakazo kuwa tumeamua baada ya Katiba mpya kuanza kazi. Hivi sasa TPDC inafanya kazi hii mpaka Zanzibar jambo ambalo hata kwa akili ya kawaida halipaswi kukubalika.

Aidha, napendekeza kwamba Zanzibar ianzishe Shirika lake la Mafuta sasa. Jambo hili halina haja ya kusubiri vikao vya kero za Muungano kwani ni dhahiri TPDC haina mamlaka,ushawishi na uthubutu kusema uhalali wa kusimamia vitalu vya Mafuta vilivyopo  Zanzibar.

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ipeleke muswada katika Baraza la Wawakilishi kuanzisha Shirika la Mafuta na Gesi la Zanzibar (Petroleum Corporation of Zanzibar – PetroZan) ili liweze kushiriki katika utafutaji na uchimbaji wa Mafuta Zanzibar. Lakini Pia PetroZan ilinde maslahi ya Zanzibar katika tasnia hii kwa kujijengea uwezo wa kusimamia ugawaji bora wa Mapato kutoka katika Mafuta na Gesi Asilia.

Kama Serikali ya Mapinduzi Zanzibar inachelea kuanzishwa kwa Shirika hili, Wawakilishi wa pande zote (CCM na CUF) wapeleke muswada binafsi kuunda Shirika la Mafuta la Wazanzibari. Hawatakuwa wamevunja Katiba ya Muungano kwani hivi sasa hakuna Taasisi yenye mamlaka ya kusimamia Tasnia hii kwa Upande wa Zanzibar.

Wakati haya yote yanafanyika, shughuli za utafutaji Mafuta na Gesi katika vitalu vilivyopo katika eneo la Zanzibar na hasa vitalu namba 9,10,11 na 12 na katika kitalu cha kati ya Pemba na Tanga ziendelee kufuatia marekebisho ya Mkataba wa Utafutaji. Utafutaji wa Mafuta una faida zaidi kwa Nchi hizi mbili kuliko kwa Kampuni za Mafuta kwani uwekezaji wa Kampuni pekee na nchi zitapata taarifa za kijiolojia zitakazosaidia mikataba ya baadaye kuwa bora zaidi.

Wakati nasisitiza kwamba tuendelee na utafutaji katika vitalu tajwa, katika Katiba mpya, utafutaji wa mafuta usimamiwe na Taasisi ya Muungano. Uchimbaji na biashara ya Mafuta ufanywe na kila Serikali ya kila upande wa Muungano. Mafuta kuwa jambo la Muungano halafu kusimamiwa na Shirika la Tanganyika na Wizara ya Upande mmoja ya Muungano ndio chanzo cha mgogoro. Suluhisho sio kuifanya TPDC kuwa Shirika la Muungano, bali kila upande upewe uhuru wa kusimamia uchimbaji, Biashara na mlolongo mzima wa tasnia ya Mafuta (value chain from midstream to downstream) isipokuwa utafutaji (upstream). Hili ndio suluhisho la kudumu ninaloona linafaa. 

Uwazi (declaration):

Zitto Kabwe ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini na mfuatiliaji wa karibu wa Tasnia ya Mafuta na Gesi Asilia akiwa amesomea mfumo wa uchumi wa katika tasnia ya madini na mafuta (fiscal regime in Mineral and Petroleum sector).  Zitto pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma ambayo inasimamia mahesabu na utendaji wa Shirika la TPDC. Makala hii imeandikwa baada ya ziara ya Mafunzo ya Wabunge kutembelea nchi ya Uholanzi kwa ufadhili wa Wizara ya Mambo ya Nje ya nchi hiyo. Katika ziara hiyo Wabunge hao walikutana na Wakuu wa Shirika la Mafuta la Shell ambapo walizungumzia pia suala la vitalu namba 9, 10, 11 na 12.