Zitto na Demokrasia

Zitto na Demokrasia

Posts Tagged ‘NCCR

RUZUKU YA VYAMA VYA SIASA

with 2 comments

Msajili wa Vyama vya Siasa-Jaji Francis S.K.Mutungi

Msajili wa Vyama vya Siasa-Jaji Francis S.K.Mutungi

Shilingi bilioni 67.7 zimelipwa na Serikali kwa vyama vya siasa katika kipindi cha miaka 4, 2009/2010 mpaka 2012/2013. Fedha hizi hazijakaguliwa kwa mujibu wa Sheria.

Mahesabu ya Vyama vya siasa nchini yanapaswa kukaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Mahesabu ya Serikali kwa mujibu wa Sheria tangu mwaka 2009. Tangu mwaka huo Kamati ya PAC haijawahi kuona Taarifa ya CAG kuhusu ukaguzi wa vyama vya siasa. Nilihoji tangia Aprili 2011 https://zittokabwe.wordpress.com/category/ruzuku-vyama-vya-siasa/

Kamati imemwita Msajili wa vyama ili kufafanua ni kwa nini Vyama vya Siasa nchini havifuati sheria (vifungu vya sheria vimeambatanishwa hapa chini). Uvunjifu huu wa Sheria ni wa makusudi au wa kutokujua? Sheria inataka Mahesabu ya vyama yatangazwe kwa uwazi, tena kwa Government Notice. Umewahi kuona? Tarehe 15 Oktoba, 2013 Kamati ya PAC itatafuta majibu haya kutoka kwa Msajili na ikibidi vyama vyenyewe. Tunataka uwazi wa matumizi ya Fedha za Umma.Vyama vya siasa ndio vinaunda Serikali, uwazi unaanzia huko ili kuepuka fedha chafu kama za EPA kuingia kuvuruga uchaguzi.

Vyama vifuatavyo vimepokea Ruzuku ya jumla shilingi bilioni 67.7 tangu mwaka wa fedha 2009/2010;

  • CCM tshs 50.97 bilioni
  • CHADEMA tshs 9.2 bilioni
  • CUF tshs 6.29 bilioni
  • NCCR – M tshs 0.677 bilioni
  • UDP tshs 0.33 bilioni
  • TLP tshs 0.217 bilioni
  • APPT – M tshs 11 milioni
  • DP tshs 3.3 milioni
  • CHAUSTA tshs 2.4 milioni

Political Parties Act, No. 5 of 1992 as ammended from time to time.

14. -(1) Every political party which has been fully registered shall—
a) maintain proper accounts of the funds and property of the party;
b) submit to the Registrar –

“(i) an annual statement of the account of the political party audited by the Controller and Auditor-General and the report of the account.” (This became law in March, 2009)

ii) an annual declaration of all the property owned by the party.

(2) The Registrar, after inspecting any accounts or report submitted pursuant to this section may, for the benefit of the members or the public, publish any matter relation to the funds, resources or property of any party or the use of such funds, resources or property.

(3) The Registrar shall publish in the official Gazette, an annual report on the audited accounts of every party.

18. -(1) Subventions granted to a party may be spent only on

(a) the parliamentary activities of a party;
(b) the civil activities of a party;
(c) any lawful activity relating to an election in which a party nominates acandidate;
(d) any other necessary or reasonable requirement of a party.

(2) Subventions granted to a political party shall be accounted for to the Registrar, separately from the accounting for other funds of the party.

(3) Any party which fails or neglects to account for subventions in accordance with this Act, shall forfeit the right to any subsequent subvention due to the party in accordance with this Act.

(4) Where the Registrar is for any reasonable cause, dissatisfied with any account of subventions submitted by any party, so much of the subvention which has not been accounted for or has not been accounted for satisfactorily, shall be deducted form any subsequent subvention due to the party.

(5) If by reason of failure to submit an account or for any other reason, the Registrar has reason to suspect that any offence under the Penal Code may have been committed in relation to the money which has not been committed in relation to the money which has not be been accounted for, he may make a report to a police station, and the officer in charge of that police station shall cause the matter to be investigated.

18A. Notwithstanding the provisions of sections 14 and 18, every political party receiving subvention in accordance with this Act shall, not later than 3151
October every year, submit to the Registrar financial statements and audited accounts reflecting any other source of funds and details regarding the manner in which such funds were used.” (became law in 2009)

Posho za wabunge zapanda kimyakimya

with 8 comments

ZAPANDA KUTOKA SH70,000 HADI 200,000, NI ZAIDI YA ASILIMIA 150
Fredy Azzah

Bunge Letu

HUKU mjadala wa kufutwa au kwa posho za wabunge na watumishi wengine wa Serikali ukiwa umefifia, posho za vikao (sitting allowance) za wabunge zimepanda kutoka Sh70,000 kwa siku hadi Sh200,000, imefahamika.

“Zimeongezeka kutoka Sh70,000 mpaka 200,000, wameanza kulipwa Bunge lililopita hili ni ongezeko la karibu mara tatu, yaani asilimia 154,” kilieleza chanzo chetu kutoka ndani ya Ofisi za Bunge.

Kutoka na ongezeko hilo, kwa sasa kila mbunge atakuwa akilipwa Sh80,000 ikiwa ni posho ya kujikimu (perdiem) anapokuwa nje jimbo lake, posho ya vikao (sitting allowance) Sh200,000 na mafuta ya gari Sh50,000 kila siku, ambazo jumla yake ni Sh330,000 kwa siku.

Kutokana na ongezeko hilo, Bajeti ya Bunge kwa ajili ya posho za vikao vya wabunge imepanda na kufikia Sh28 bilioni kwa mwaka.

Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashililah alipoulizwa kuhusu taarifa hizo alisema hawezi kuzungumzia jambo hilo kwa sababu siyo msemaji wa wabunge, bali Ofisi ya Bunge.

“Ni nani kawapa hizo taarifa bwana, au ni vyanzo vyenu vya habari?” alihoji Dk Kashililah.

Baada ya kuelezwa kuwa taarifa hizo zimetoka kwenye vyanzo vyetu vya kuaminika alisema “Hao wana utaratibu wao bwana, labda mtafute Spika ndiye msemaji wa Wabunge.”

Juhudi za kumpata Spika, Anne Makinda kutoa ufafanuzi wa suala hili, hazikufanikiwa baada ya simu yake kuita wakati wote bila kupokewa hata pale alipotumiwa ujumbe mfupi wa simu (sms) hakujibu. Hata simu zote za Naibu wake, Job Ndugai hazikupatikana.

Hata hivyo, Mbunge wa Ludewa (CCM), Deo Filikunjombe alisema kuongezeka kwa posho hizo kunatokana na wabunge kuwa wanalipwa mishahara midogo kulingana na kazi wanayofanya.

Alisema endapo wawakilishi hao wa wananchi wangekuwa wanalipwa mishahara inayolingana na kazi wanayofanya, kusingekuwa na sababu ya kuongezeka kwa posho hizo.

“Ninachosema mimi, siyo wabunge peke yao, lakini watumishi wote wa umma wanalipwa mishahara midogo sana mimi binafsi sitegemei posho za Bunge, kabla ya kuingia bungeni nilikuwa nimefanya kazi kwa miaka 14 na nilikuwa napata mshahara mzuri tu,” alisema Filikunjombe.

Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema), Mchungaji Peter Msigwa alisema amezisikia taarifa hizo za kuongezeka kwa posho lakini siyo kwa undani. Hata hivyo alisema hakuwa katika nafasi nzuri ya kuzungumza suala hilo.

Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe alisema walivyokuwa wakipinga posho hizo wakati zilivyokuwa Sh70,000 waandishi wa habari walichukua suala hilo kama ajenda ya Chadema, hivyo kupandishwa kwa posho hizo ni matokeo ya watu kuwapuuza walivyokuwa wakizipinga.

“Msimamo wetu sisi tulishautoa tangu wakati posho zikiwa Sh70,000 wakati sisi tukipinga hizi posho waandishi wa habari na Watanzania mlichukulia suala hili kama ajenda ya Chadema, sisi wenyewe tupo wachache bungeni, tulichotaka ni kuonyesha jinsi fedha za Watanzania zinavyotumika vibaya,” alisema na kuongeza:

“Achilia mbali hizo 200,000 za wabunge kuna watu huko serikalini wanalipwa mpaka Sh400,000 au Sh1 milioni kwa siku nyie ulizeni.”

Alipoulizwa kama amechukua posho hiyo ya Sh200,000 alisema hajafanya hivyo kwa sababu hazifuatilii.

“Sijui hata kama zimeanza kulipwa au la kwa sababu huwa sizifuatilii na haka kama suala la posho hilo zilijadiliwa wakati wa vikao vya mwanzo mimi sikuwepo kwa sababu tulikuwa kwenye kesi yetu Arusha na bungeni tulikuja mwishoni wakati wa Muswada wa Katiba,” alisema Mbowe.

Ongezeko hili la posho za wabunge limekuja wakati Watanzania wakiendelea kuishi kwenye maisha magumu yanayochangiwa na mfumuko wa bei ambao mpaka mwisho mwa Oktoba ulikuwa umefikia asilimia 17.9.

Pia ongezeko hili limekuja wakati Watanzania wakiwa na matumaini ya posho hizi kupunguzwa baada ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kutangaza bungeni kuwa Serikali imekubali pendekezo la kutafakari na kuziangalia upya posho mbalimbali wanazolipwa wabunge na watumishi wote umma.

Mbunge wa Muhambwe (NCCR-Mageuzi), Felix Mkosamali alisema kuwa hawezi kuzungumza chochote juu ya posho hizo kwa kuwa hajapata barua rasmi juu ya kupanda kwake.

“Sijapata barua yoyote, nikiuliza na kupata majibu kwa wahusika nitakuwa na uhakika na nitakupa maoni yangu na msimamo wangu vizuri kabisa, lakini kwa sasa siwezi kusema chochote,” alisema Mkosamali.

Juni 7, mwaka huu Naibu Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni Zitto Kabwe, aliwasilisha barua Ofisi ya Bunge akikataa posho akisema watumishi wa Serikali na wabunge, hawastahili kulipwa posho wanapohudhuria vikao rasmi vya uwajibikaji wao wa kawaida.

Zitto alisema posho hiyo haistahili kulipwa kwake, wabunge wengine wala watumishi wa umma kwa kuwa kuhudhuria vikao ni sehemu ya kazi zao.

Alisema kitendo cha Waziri Mkuu kueleza kuwa watatafakari na kuangalia upya na kwamba suala la posho ni sera ya taifa na Ilani ya Uchaguzi ya CCM, ni ishara ya kiongozi huyo wa juu kukubali wazo la Chadema na safari ya kufuta posho hizo.

Awali, mara baada ya Chadema kutangaza msimamo huo, Spika Makinda alipinga uamuzi wa kususia posho akisema suala hilo lipo kisheria na kwamba hakuna mtu ambaye anaweza kuamua kuliondoa.

Alisema wabunge wa Chadema wataendelea kulipwa posho za vikao kupitia akaunti zao za benki na watatakiwa kusaini fomu ya mahudhurio ya Bunge, vinginevyo watajiweka katika wakati mbaya.

Hata hivyo, akihitimisha hoja za wabunge katika hotuba yake ya makadirio ya matumizi ya ofisi yake na zilizo chini yake juzi, Pinda alisema suala la posho lipo kwenye mchakato wa kuangaliwa upya.

Source: Mwananchi

Written by zittokabwe

November 28, 2011 at 9:38 AM

Muswada wa Marekebisho ya Katiba ujenge Mwafaka wa Kitaifa

with 14 comments

Zitto Kabwe[1], Mb

Kama kuna jambo moja ambalo huunganisha Taifa ni Katiba ya Taifa hilo. Katiba huweka misingi mikuu ya nchi na namna ya kujenga na kuendesha Taifa. Hivyo Katiba inapaswa kuwa ni matokeo ya mwafaka wa kitaifa kwenye masuala yote ya msingi ya nchi husika. Tanzania imekuwa ikiongozwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 kama ilivyofanyiwa marekebisho mara kwa mara. Kabla ya hapo kulikuwa na Katiba ya Uhuru ambayo ilitokana na Mwafaka wa wapigania Uhuru wa nchi yetu, baadaye Katiba ya Jamhuri ya Tangayika na kisha Katiba ya muda ya Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kabla ya kubadili jina na kuitwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Ukiachana na Katiba ya Uhuru, Katiba nyingine zote hazikutokana na mwafaka wa kitaifa bali matakwa ya tabaka la watawala. Katiba ya kudumu ya mwaka 1977 ni zao dhahiri kabisa la utawala wa chama kimoja ambacho kilikuwa na dhamira ya kushika hatamu za uongozi. Kutokana na hali hii haikuchukua muda kwa wasomi mnamo mwaka 1983 kuanza harakati za kuifanyia mabadiliko makubwa. Mabadiliko hayo yalizaa kuwemo kwa Haki za Msingi za Binaadamu katika Katiba katika mabadiliko ya mwaka 1984, miaka saba tu toka kuandikwa kwa Katiba ya kudumu.

Takribani mwaka mzima huu kumekuwa na madai ya kuandikwa kwa Katiba mpya. Madai haya sio mapya kwani huibuka na kusinyaa kila baada ya uchaguzi Mkuu. Itakumbukwa kwamba miaka ya Tisini mwishoni kundi la vyama vya siasa liliunda Kamati ya Mabadiliko ya Katiba (KAMAKA) ili kudai kuandikwa kwa Katiba mpya. Hata hivyo safari hii sauti ya mabadiliko imekuwa ni kubwa sana kiasi cha Serikali kusikia na hivyo kupeleka Bungeni muswada wa Marejeo ya Katiba kwa lengo la kuandika Katiba mpya ya nchi yetu. Muswada huu umeleta kelele nyingi na manung’uniko mengi sana kutoka kwa makundi mbalimbali ya jamii kuanzia vyama vya siasa, viongozi wa dini na Asasi za Kijamii. Baadhi ya Asasi za Kijamii zimeunda Jukwaa la Katiba ili kuweza kuratibu vizuri juhudi za kuandikwa kwa Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Sababu kubwa ya kupingwa kwa muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya mwaka 2011 ni kwamba mchakato umewekwa kwenye Dola mno na hasa kwenye Urais. Rais anateua Tume ya kukusanya maoni, Rais anateua Bunge la Katiba nk. Watu wengi tungependa kuona mchakato unakuwa kwa wananchi zaidi. Serikali imefanya marekebisho kadhaa na kupanua wigo wa mjadala wa Katiba na pia kumhusisha kikamilifu Rais wa Zanzibar katika mchakato.

Baadhi yetu tunaona kama nafasi ya Zanzibar katika mchakato imepewa nguvu kubwa kupita kiasi. Ninadhani Zanzibar inastahili kupata nafasi hii katika mchakato wa Katiba. Jambo ambalo ni vizuri tulitilie maanani ni kwamba Muungano wa Mwaka 1964 ulihusisha nchi mbili huru zenye hadhi sawa mbele ya sheria za kimataifa. Linapokuja suala la kuandika Katiba ya Muungano, pande mbili za Muungano zinakuwa na hadhi sawasawa. Kwamba Zanzibar ishiriki kwenye masuala ya Muungano tu ni hoja inayojadilika iwapo tu Katiba ya Muungano ingetofautisha kinagaubaga taasisi za kimuungano na zisizo. Kwa mfano Sura ya Bunge katika Katiba ni lazima ijadiliwe na pande zote mbili ingawa Bunge wakati mwingine hupitisha miswaada ambayo sio ya masuala ya Muungano. Aina ya Muungano wetu inatulazimisha kufanya hivi tunavyofanya sasa. Mkataba wa Muungano ni lazima uheshimiwe kama ulivyo sasa.

Katiba mpya yaweza kuweka makubaliano mapya lakini muswada wa sasa ni lazima utambue nafasi halali ya Zanzibar kwa mujibu wa Katiba ya sasa na Hati za Muugano. Suala hili ni suala la kisheria na sio suala la idadi ya watu au ukubwa wa eneo la nchi husika. Nchi ya Ushelisheli yenye watu 80,000 ina nafasi sawa na Tanzania yenye watu 42 milioni katika SADC, AU na UNO. Zote zina kura moja tu. Huu ndio ukweli na hatuna budi kukubaliana nao.

Muswada unampa mamlaka Rais wa Tanzania na Rais wa Zanzibar kuteua Tume ya Katiba. Tume hii maRais hawatapata ushauri wa mtu mwingine yeyote  kwa mujibu wa kifungu cha (6) na vifungu vidogo (1), (2) na (3). Wanasiasa wakiwemo Wabunge, Wawakilishi, viongozi wa vyama wa Ngazi za Taifa, Mkoa au Wilaya hawatakuwa na sifa za kuteuliwa.

Inawezekana kabisa waandishi wa muswada walikuwa na mantiki ya kuuondoa mchakato kwenye mikono ya wanasiasa. Nia hii njema haikufikiriwa vizuri hata kidogo. Njia hii haijengi mwafaka. Tume hii sio ya Wataalamu, ni Tume inayopaswa kuwa na sura ya kitaifa. Nafasi ya wanasiasa katika mchakato wa kukusanya maoni ni muhimu sana katika kuhalalisha mchakato wenyewe. Tume lazima ionekane ni Tume ya Taifa na sio Tume ya maRais. Hivyo kipengele hiki cha kuwanyima sifa wanasiasa kinapaswa kufutwa katika muswada. Wabunge na Wawakilishi kwa kuwa ni sehemu ya Bunge la Katiba wasiwemo katika Tume, lakini viongozi wengine wa kisiasa wawe na haki ya kuteuliwa kuwa wajumbe.

Lakini pia Rais ateue Tume kutokana na maoni kutoka katika makundi yenye maslahi ya karibu na Katiba ya nchi na hivi ni vyama vya siasa. Ninapendekeza kwamba katika Wajumbe 30 wa Tume ya kukusanya maoni ya Katiba, 10 watokane na vyama vya siasa vyenye Wabunge kwa uwiano wa CCM 2, CHADEMA 2, CUF 2, NCCR 2, TLP 1 na UDP 1. Kila chama cha siasa chenye Wabunge kupitia kiongozi wake Bungeni kipeleke majina ya watu wanaowapendekeza kuwa katika Tume ya Katiba na kutokana na Mapendekezo hayo Rais atawateua kuwa wajumbe. Masharti mengine ya nusu kutoka kila upande wa Muungano yazingatiwe.

Muswada unapendekeza kuwepo kwa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Tume. Kifungu cha cha 7 kifungu kidogo (1), (2) na (3) kinaweka utaratibu wa kupatikana kwa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Tume. Muswada unasema UTEUZI wa Mwenyekiti na Makamu utazingatia kwamba mmoja atoke uapnde mmoja wa Muungano na mwingine upande wa Pili wa Muungano. Ingawa Muswada hausemi waziwazi lakini ni dhahiri kwamba Mwenyekiti wa Tume atateuliwa na Rais baada ya kushauriana na kukubaliana na Rais wa Zanzibar. Sitaki kujenga hoja kwamba Mwenyekiti na Makamu wachaguliwe na wajumbe wa Tume kutoka miongoni mwao lakini ni dhahiri Mwenyekiti wa Tume anapaswa kuwa mtu mwenye heshima kubwa hapa nchini. Ningependekeza kwamba maRais wateue Wenyeviti wenza badala ya Mwenyekiti na Makamu wake ili kuweka nafasi sawa kwa pande mbili za Muungano. Hapa nchini tunao Watanzania ambao wamefanya kazi iliyotukuka katika nyadhifa mbalimbali na sasa ni wastaafu wasio na nia yeyote ya madaraka ya kisiasa wanaoweza kuongoza vizuri kabisa Tume hii. Ni pendekezo langu kwamba Dkt. Salim Ahmed Salim na Jaji Joseph Sinde Warioba wawe wenyeviti wenza wa Tume ya Katiba. Uzoefu wao katika uongozi na kuijua kwao nchi kutasaidia sana kuhakikisha kwamba mchakato wa kukusanya maoni na kisha kuandika Katiba unakuwa na mafanikio kwa kuzingatia misingi ya Taifa letu.

Muswada unapendekeza kwamba Hadidu rejea za Tume zitolewe na maRais. Kifungu cha nane na muswada kuhusu hadidu rejea nadhani hakina mantiki sana. Madhumuni ya muswada yanasema pamoja na mambo mengine muswada unaweka masharti kuhusu Hadidu rejea za Tume. Wakati huo huo muswada unasema Hadidu rejea zitakuwa ni hati ya kisheria itakayozingatiwa na Tume katika kazi zake.

Mantiki ni kwamba Hadidu rejea zinapaswa kuwa sehemu ya Muswada kama ‘schedule’ ili kuzipa nguvu ya kisheria badala ya tangazo katika gazeti la Serikali. Hadidu rejea zikiwa ni sehemu ya Muswada zitajadiliwa na Bunge na kupitishwa hivyo kuwa ni jambo ambalo limefikiwa kwa mwafaka wa wawakilishi wa wananchi.

Muswada unataka uamuzi wa kura ya maoni kuhusu Katiba uwe ni kukubaliwa na nusu ya Watanzania katika kila upande wa Muungano. Nadhani hapa tunacheza na Katiba ya nchi. Katiba ya nchi inapaswa kukubaliwa na theluthi mbili ya wapiga kura wa pande zote za Muungano yaani kila upande theluthi mbili. Hii itaipa Katiba ‘legitimacy’ na hivyo kuheshimiwa na wananchi na watawala. Kuna woga gani uliopo kutaka katika ikubalike na nusu ya wapiga kura? Mifano ya nchi nyingi duniani Katiba inapaswa kukubaliwa na theluthi mbili ya wapiga kura. Hata jirani zetu wa Kenya ilikuwa hivyo na hata kura ya maoni kuhusu mwafaka huko Zanzibar ilikuwa hivyo. Kwa kuwa Katiba ni chombo cha mwafaka wa kitaifa, muswada utamke kwamba Katiba mpya itakuwa imepita iwapo theluthi mbili ya wapiga kura watapiga kura ya ndio.

 mwisho


[1] Zitto Kabwe ni Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kaskazini na Naibu Katibu Mkuu CHADEMA. Maoni haya ni maoni binafsi ya Zitto na kwa vyovyote vile hayawakilishi msimamo rasmi wa CHADEMA au Kambi ya Upinzani Bungeni.

Written by zittokabwe

November 7, 2011 at 11:52 AM