Zitto na Demokrasia

Zitto na Demokrasia

Posts Tagged ‘MEM Tanzania

Maandamano dhidi ya Bomba la Gesi: Kilio cha Uwajibikaji

with 24 comments

Maandamano dhidi ya Bomba la Gesi: Kilio cha Uwajibikaji

Maandamano dhidi ya Bomba la GesiPicha Hisani ya: Mtwara Kumekucha Blog by Baraka Mfunguo

Maandamano dhidi ya Bomba la Gesi
Picha Hisani ya: Mtwara Kumekucha Blog by Baraka Mfunguo

‘Dar inachangia asilimia 80 ya mapato. Kitovu cha Uchumi. Dar inachangia 90% ya ufisadi. Uti wa mgongo wa ufisadi nchini’

Malumbano kati ya wananchi wa Mtwara na Serikali kuhusu matumizi bora ya utajiri wa nchi yameendelea kwa takribani wiki moja sasa. Baada ya Mkuu wa Mkoa wa Mtwara na Waziri wa Nishati na Madini kuwaita Watanzania wa Mtwara Wahaini, wapuuzi na watu hatari, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania naye aliingia kwenye mjadala huo kwa kuonya watu wanaowaunga mkono watu wa Mtwara na kuwaita watu wanaotafuta umaarufu wa kisiasa na wanaotaka kugawa nchi. Siku moja baada ya hotuba ya Rais, Waziri wa Nishati na Madini alifanya mkutano na waandishi wa habari kueleza suala lile lile ambalo bosi wake alilielezea usiku wa kuamkia mwaka mpya 2013. Hii ni dalili ya Serikali kuweweseka.

Katika kauli ya Serikali, ambayo haikuwa na jipya zaidi ya wimbo ule ule wa ‘kugawa nchi’ ‘umaarufu wa kisiasa’ nk, Serikali ilitaka kuonyesha umma kuwa watu wa Mtwara hawana shukurani. Kwamba miaka yote toka Uhuru watu wa Mtwara wamekuwa wakilishwa na Pamba, Kahawa, Chai, Tumbaku, Sukari, Kidatu nk. Kwamba watu wa Mtwara na Lindi hawakuchangia hata kidogo kwenye hazina ya Taifa. Hivyo wao kupigia kelele gesi yao ni uchoyo na roho mbaya na kukosa shukurani. Kauli ya Serikali ni kauli ya chombo kinachoendelea kukosa ‘legitimacy’ ya kuongoza taifa. Ni kauli ya kukata tamaa. Ni kauli hatari sana dhidi ya Watanzania waliojitolea damu kulinda uhuru wa nchi yetu.

Moja, Serikali katika kauli yake haitaji kabisa kwamba toka Uhuru watu wa Mtwara na Lindi wamekuwa wachangiaji wakubwa sana katika uchumi wa Taifa kupitia zao la Korosho. Takwimu za Uzalishaji wa Korosho zinaonyesha kwamba kuanzia mwaka 1965 mpaka 2011 Korosho imeliingizia Taifa fedha kigeni jumla ya dola za Kimarekani 4.58 bilioni ( Cashewnuts Sub-sector study 2003, Hali ya Uchumi 2012, Cashewnuts Tanzania Report 2010). Katika Mwaka wa Uchumi unaoishia Novemba 2012, Korosho imeliingizia Taifa jumla ya dola za Kimarekani 151 milioni. Katika mwaka 2011 zao hili liliingiza dola 130 milioni wakati Pamba iliingiza dola 53 milioni tu. Licha ya Zao la Korosho kuingiza fedha hizi za kigeni  (sawa ni shilingi trilioni 7.2) kwa nchi mikoa ya Lindi na Mtwara ipo miaka 50 nyuma kimaendeleo kulinganisha na mikoa mingine ya Tanzania. Serikali inataka kufuta historia ya mchango wa zao la Korosho kwenye uchumi wa nchi yetu kwa sababu ya uroho wa gesi asilia. Kwa nini kauli rasmi ya Serikali haijataja Korosho kabisa? Kauli hii ilipitishwa na ngazi zote za Serikali? Mawaziri wa Serikali wanaotoka mikoa ya Lindi na Mtwara walikubali kauli kama hii itoke dhidi ya wananchi wao wanaoteseka na zao la Korosho miaka nenda miaka rudi?

Pili, Serikali imesahau kabisa mchango wa watu wa Lindi na Mtwara katika ulinzi wa Taifa letu. Moja ya sababu ya mikoa ya Lindi na Mtwara kuwa nyuma kimaendeleo ni juhudi za ukombozi wa kusini mwa Afrika. Kambi ya wapigania uhuru wa Msumbiji ilikuwa Nachingwea. Kambi ya Frelimo iliwekwa kwenye Shamba la Mkonge kilometa 17 tu kutoka mjini Nachingwea ambapo ilikuwa makao makuu ya ukombozi wa Msumbiji. Rais Samora Machel, Rais Joaqim Chissano na Rais Guebuza waliendesha mapambano kutoka kusini mwa Tanzania. Makaburu wa Afrika Kusini na Wareno walikuwa wanashambulia nchi yetu na mikoa hii miwili ya Lindi na Mtwara ikawa ‘buffer zone’. Wakati Dar es Salaam inaendelea kwa kila aina ya maendeleo, mikoa ya Lindi na Mtwara ilikuwa inalinda ili wanaoishi Dar es Salaam na mikoa mingine waishi wa amani na starehe. Serikali inapimaje mchango huu wa mikoa hii? Tunaipima kwa fedha? Uroho wa gesi asilia kuzalisha umeme wa kufurahisha walalaheri asilimia 14 nchini ndio inaifanya Serikali kusahau kabisa ‘sacrifice’ ya watu wa Mtwara katika kulinda uhuru wa Taifa letu?

Tatu, Serikali inasema lazima bomba lije Dar es Salaam kwa sababu Dar ndio inazalisha asilimia 80 ya Mapato ya Serikali. Kwanza huu ni uwongo. Ni aibu Serikali kujitetea kwa uwongo. Dar es Salaam ni kituo tu cha kukusanyia mapato ya Serikali. Uzalishaji mkubwa wa nchi yetu wenye kuzalisha kodi unafanyika nje ya Dar es Salaam. Walipa kodi wakubwa wengi Ofisi zao Kuu zipo Dar es Salaam lakini uzalishaji wao unafanyika nje ya Dar es Salaam. Serikali itoe orodha ya walipa kodi wakubwa 100 tuone uzalishaji halisi wa mapato hayo unafanyika wapi. Hata hivyo inawezekana kuwa ikawa kweli Dar es Salaam inakusanya asilimia 80 ya mapato ya nchi. Basi na tuseme Dar es Salaam inachangia asilimia 90 ya ufisadi wote nchini. Kashfa zote kubwa za Ufisadi zinafanyika Dar es Salaam na fedha nyingi za ufisadi zinatumika Dar es Salaam.

Mwisho, maandamano ya watu wa Mtwara ni kielelezo tosha kwamba watu wa mikoa ya Lindi na Mtwara wamechoshwa na longolongo za Serikali. Wananchi wa Mtwara na Lindi wanataka Uwajibikaji wa Serikali kuhusu utajiri wa nchi. Mtanzania yeyote mwenye tahadhari ya nchi yetu kutokuwa na laana ya rasilimali ataungana mkono na watu wa Lindi na Mtwara kudai maendeleo. Nilitoa mfano wa Mgodi wa Golden Pride ambao umemaliza dhahabu yote tani 76 katika eneo la Lusu wilayani Nzega. Kampuni ya Resolute ya Australia iliwekeza dola 370 milioni kuanzia mwaka 1998 (mkataba wao ulisainiwa 25th June 1997). Katika kipindi cha uhai wa mgodi, miaka 14,  Kampuni hii imeuza dhahabu ya thamani ya dola za kimarekani 3.3 bilioni. Kabla Serikali haijawaita watu Mtwara wahaini, wapuuzi na watu hatari, iwaambie watu Watanzania kodi kiasi gani imekusanywa kutoka mgodi huu katika kipindi cha miaka 14. Mpaka mwaka 2008, kwa mujibu wa Taarifa ya Kamati ya Bomani, kampuni hii ilikuwa imelipa mrahaba wa dola 11 milioni na kodi nyingine dola 16 milioni. Serikali itwambie ilipofika Disemba 2012 kodi kiasi imekusanywa kutoka kampuni hii?

Pia watu wa Mtwara na Lindi wameona historia ya bomba la Songosongo. Hata kodi ya Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa (0.3%) ilikuwa inalipwa Halmashauri ya Manispaa Ilala na kampuni ya Pan Africa Energy. Ilichukua juhudi za mbunge wa Kilwa Kaskazini Murtaza Mangungu kuingilia kati ndio kodi ikaanza kulipwa Kilwa ambapo uzalishaji unafanyika. Watu wa Mtwara ni werevu, wanajua wafanyalo. Wanataka utajiri wa nchi unufaishe nchi kwa kuanzia kule utajiri ulipo. Kuna dhambi gani?

Uwajibikaji katika uvunaji wa Rasilimali ya Gesi ndio chanzo cha maandamano ya watu wa Mtwara. Serikali isikimbilie kulaumu wanasiasa kwamba ndio wamechochea maandamano haya. Haya ni maandamno ya wananchi wakitaka Serikali yao iwajibike kwao. Serikali ithubutu kufanya ubabe wa kujenga bomba la gesi bila ridhaa ya Wananchi wa Lindi na Mtwara. Wananchi wanapohitaji uwajibikaji ni wajibu wa Serikali kuwajibika kwao ni sio kuwaita wahaini, wachochezi, watu hatari, wapuuzi. Watu wa Mtwara wamechangia maendeleo ya Taifa letu kwa jasho na damu. Serikali ina wajibu wa kuwasikiliza, kuwaelimisha na kupata mwafaka. Kauli ya Serikali imewatukana watu wa Mtwara na Lindi. Hawatakubali kudhalilishwa. Hawatakubali historia yao kufutwa. Hawatakubali waendelee kubaki nyuma kimaendeleo. Serikali ifikirie tena.

Written by zittokabwe

January 3, 2013 at 2:10 PM

PRESS RELEASE: Shilingi Bilioni 86 zaibwa Wizara ya Nishati/TANESCO, Gridi ya Taifa hatarini

with 36 comments

Shilingi bilioni 86 zaibwa Wizara ya Nishati/TANESCO, Gridi ya Taifa hatarini

Gazeti la The East African la Novemba 24 – 30, 2012 limetoa taarifa kwamba jumla ya dola za kimarekani milioni 54 zimegundulika kuibwa na watumishi waandamizi wa Wizara ya Nishati na Madini na Shirika la TANESCO kupitia manunuzi ya Mafuta ya kuendesha mtambo wa Umeme wa IPTL. Gazeti hili limenukuu taarifa ya ukaguzi kutoka kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Tanzania (Controller and Auditor General). Taarifa hiyo inasema kuna kikundi (racket) ambacho kazi yake kubwa ni kujifaidisha binafsi na mpango wa umeme wa dharura kupitia manunuzi ya Mafuta mazito ya IPTL.

Itakumbukwa kwamba toka mwaka 2011 kumekuwa na shinikizo lililotolewa na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma, Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini na Waziri Kivuli wa Nishati na Madini kwamba zabuni za ununuzi wa mafuta ya kuendesha mpango wa umeme wa dharura na mchakato mzima wa manunuzi ya mafuta haya ufanyiwe uchunguzi wa kina (forensic audit).

Katika mkutano wa 3 wa Bunge la Kumi (April 2011) niliuliza swali Bungeni kuhusu kashfa hii ya ununuzi wa mafuta ya kuendesha mtambo wa IPTL na baadaye tarehe 16 Aprili 2011 nilimwomba Spika airuhusu Kamati ya Nishati na Madini kufanya uchunguzi kuhusu kashfa hii. Kamati ya Nishati na Madini chini ya aliyekuwa Mwenyekiti ndugu January Makamba ililitaka Bunge kuazimia kufanyika kwa uchunguzi kuhusu suala hili kwenye Taarifa yake ya mwaka 2011 iliyowasilishwa Bungeni mwezi Aprili mwaka 2012. Waziri Kivuli wa Nishati na Madini ndugu John Mnyika katika Hotuba yake ya Bajeti ya Wizara hiyo mwaka 2011 alipendekeza kufanyika kwa uchunguzi kuhusu kashfa hii pia. Juhudi zote hizo hazikuzaa matunda.

Kipindi hicho kiwango kilichokuwa kinahojiwa kuibwa ni shilingi bilioni 15 tu. Taarifa ya The East African kama walivyonukuu kutoka kwenye taarifa ya CAG inaonyesha fedha zilizoibwa ni shilingi bilioni 86.

Zabuni za kununua mafuta ya kuendesha umeme wa dharura zimekuwa zikitolewa bila kufuata utaratibu wa zabuni kwa mujibu wa Sheria ya manunuzi. Hivi sasa kila mwezi Tanzania inatumia dola milioni 70 kununua mafuta ya kuendesha mitambo ya umeme. Fedha hizi zinatoka Hazina na sehemu ndogo kutoka TANESCO. Wakati fedha hizi bilioni 112 zinachomwa kila mwezi kununua mafuta mazito na dizeli ya kuendesha mitambo ya umeme, Taarifa za kitaalamu zinaonyesha kwamba Bwawa la Mtera hivi lina kina cha maji chini ya kiwango kinachotakiwa na uzalishaji wa umeme ni asilimia 20 tu ya uwezo (installed capacity). Iwapo TANESCO wataendelea kutumia zaidi maji yaliyopo Mtera, Mitambo itashindwa kazi na Gridi nzima itasimama maana Mtera ndio nguzo kuu ya Gridi ya Taifa. Hali hii ni hatari sana kwa uchumi na ulinzi na usalama wa Taifa. Kimsingi Gridi ya Taifa ipo hatarini kutokana na kiwango cha Maji kilichopo Mtera hivi sasa na kuendelea kupungua kwa kina hicho cha maji.

Wananchi wanapaswa kuelezwa kinaga ubaga nini kinaendelea katika sekta ndogo ya umeme hapa nchini;

1.      Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali kuhusu zabuni za manunuzi ya Mafuta ya kuendesha mitambo ya umeme wa dharura iwekwe wazi na ‘racket’ inayosemekana kuiba jumla ya shilingi bilioni 86 ionyeshwe na hatua za kisheria zichukuliwe mara moja na bila kuchelewa.

2.      Waziri wa Nishati na Maadini auleze umma hali yalisi ya sekta ya umeme nchini, uzalishaji wa umeme upoje, hali ya maji katika bwawa mkakati la Mtera na nini hatma ya mitambo ya IPTL, kesi zake na utekelezaji wa mapendekezo ya Bunge kuwa kesi za kampuni hii zimalizwe nje ya mahakama. Pia Taifa lielezwe Mpango wa Dharura wa umeme unakwisha lini maana muda uliotolewa na Bunge mwezi Agosti mwaka 2011 tayari umekamilika. Waziri aeleze hatua agni amechukua baada ya kukabidhiwa taarifa na CAG kuhusu maafisa waandamizi wa Wizara waliohusika na wizi wa shilingi bilioni 86 za kununua mafuta ya IPTL.

3.      Waziri wa Fedha na Uchumi aueleze umma ni kiwango gani cha fedha Hazina imetoa kununua mafuta ya kuendesha mitambo ya umeme wa dharura kati ya Mwezi Novemba mwaka 2011 na Oktoba mwaka 2012 na kama taratibu zote za zabuni zilifuatwa na pale ambapo hazikufuatwa ni hatua gani PPRA wamechukua dhidi ya waliokiuka sheria ya manunuzi na kuleta hasara ya mabilioni ya fedha kwa Serikali.

 

Kabwe Zuberi Zitto, Mb

Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni na Waziri Kivuli wa Fedha

Dar es Salaam. Novemba 25, 2012

The Tanzania Natural Gas Policy Draft -1 #TZoil&gas #MEM

with one comment