Zitto na Demokrasia

Zitto na Demokrasia

Posts Tagged ‘Prof . Sospeter Muhongo

Sera ya Gesi: Maoni ya awali #RasimuyaGesiAsilia #TanzaniaNaturalGasPolicy

with 6 comments

Jana wabunge tumegawiwa rasimu ya Sera ya Gesi Asilia. Leo Wizara ya Nishati na Madini itaendesha semina kwa wabunge kuhusu sera hiyo.

Draft 3- The Natural Gas Policy of Tanzania -2013

Draft 3- The Natural Gas Policy of Tanzania -2013(Rasimu ya Sera ya Gesi Asilia)

Nimepata muda kidogo wa kuipitia hii rasimu ya 3 nikiwa safarini kwenda Tabora kwa shughuli za chama changu cha CHADEMA , nina maoni ya awali kama ifuatavyo;

1). Kwa ujumla kupata Sera mpya ya gesi asilia ni hatua muafaka japo imechelewa sana. Hata hivyo ni bora kuchelewa kuliko kutofika kabisa. Ni vema wananchi wachukue fursa hii kuisoma na kuijadili rasimu hii na kuiboresha ili iwezeshe wananchi wenyewe kufaidika na utajiri ambao nchi yetu imejaaliwa.

2). Sera ina jumla ya sura Sita. Sura ya kwanza ya inaweka sababu na masuala ya jumla na utangulizi . Sura ya pili inaweka sababu za kuwepo kwa sera mpya na madhumuni maalumu, Sura ya tatu ndio yenye matamko ya msingi ya kisera (fundamental policy issues) ikiwemo masuala ya miundombinu ya gesi kwa ajili ya soko la ndani, usimamizi wa mapato yatokanayo na gesi asilia na masuala ya ‘’ local content’’. Sura hii pia imezungumzia masuala ya uwazi na uwajibikaji. Sura ya nne ni masuala ya mfumo wa kisheria na udhibiti na sura ya tano ni taasisi za usimamizi wa sera ya gesi asilia. Sura ya sita ni hitimisho. Kila sura imeweka matamko ya kisera.

3). Rasimu ya sera imeshindwa kutofautisha suala la Mafuta na Gesi kuwa ni suala la Muungano au sio suala la muungano katika muktadha wa Katiba mpya inayojadiliwa sasa. Hii inadhihirisha umuhimu wa kuwianisha mchakato wa katiba na michakato mingine inayoendelea nchini. Hivi sasa Zanzibar inajiandaa kuwa na sera na sheria yao ya mafuta ya gesi, iweje sera hii itamke gesi asilia ni mali ya Jamhuri ya Muungano wakati upande mmoja wa Muungano utakuwa unafaidi utajiri wake peke yake? Rasimu ya sera imeshindwa kutambua kuwa kuna vitalu vya mafuta na gesi ya (vitalu namba 9-12) vimesimamisha shughuli kwa sababu Serikali ya Zanziabar haitambui mafuta na gesi kuwa suala la muungano. Rasimu inapaswa kuzingatia jambo hili kabla ya kupata sera yenyewe.

4). Rasimu imetamka katika ukurasa wa 9 kwamba sera hii haitambui shughuli za utafutaji (‘This policy document only covers mid-and downstream segments’ ndio nukuu ya neno kwa neon ya Sera hii). Hiki ni kichekesho cha milenia .

Taifa linawezaje kuandika sera ya gesi asilia kwa upande wa uchuuzi tu (biashara) na kuacha kazi yenyewe haswa ya utafutaji na uchimbaji (exploration and exploitation are upstream). Shughuli za utafutaji na uchimbaji ndio msingi haswa wa sera ya gesi asilia.

Mikataba yote huamuliwa kwa kuzingatia kwanza utafutaji, shughuli nyingine ni biashara tu ya kitakachogunduliwa . Rasimu kuacha kabisa eneo la utafutaji na uendelezaji (upstream) ni sawa na kutokuwa na sera kabisa.

Kwa namna eneo hili lilivyoachwa kuna harufu ya mkakati wa siri wa kuwanyima wananchi msimamo wa kisera kuhusu utajiri wao unavyonyonywa . Sentensi hii yenye maneno 10 katika uk. wa 9 wa kijitabu cha rasimu ya sera unaondoa kabisa umuhimu wa sera yenyewe wakati dhumuni kuu la sera linatamkwa uk.6 kwamba Gesi asilia ni mali ya wananchi wa ‘Jamhuri ya Muungano’ wa Tanzania’’ kurasa tatu baadaye zinaiondoa sera kwenye eneo hilo la umiliki wa mali hii ( Upstream). Tumeamua kuandika sera ya uchuuzi wa gesi asilia?

5). Rasimu katika 3.2.2(uk.24) imeweka matamko ya kisera kuhusu uwazi na uwajibikaji . Uwazi ndio eneo ambalo watanzania wengi walikuwa wanasubiri kwa hamu sana . Usiri wa mikataba katika sekta mbali mbali nchini ni chanzo cha ufisadi na uporaji wa utajiri wa mali yetu. Sera hii imeJibu swala hili? HAPANA. Sera haisemi ni namna gani mikataba itakuwa wazi kwa wananchi. Sera haisemi ni namna gani wananchi wataiwajibisha Serikali na vyombo vyake (Accountability) kwenye masuala ya mafuta na gesi. Sera imepiga porojo kuhusu uwazi na uwajibikaji. Bila misingi imara ya Uwazi na Uwajibikaji katika rasilimali ya gesi asilia, sera haina maana yoyote ile.

6). Serikali ni lazima ijue kwamba hivi sasa nchi yetu nchi tajiri yenye watu masikini.[i] sera ya gesi inapaswa kutuondoa kuwa nchi yenye laana ya rasilimali. Sera hii haina mwelekeo huo kabisa . Sera inapaswa kuwezesha wananchi kupata thamani ya maliasili yetu na kuwezesha matumizi mazuri ya mapato yatokanayo na utajiri wa nchi.

Sera yetu lazima ioneshe dhahiri kwamba gesi asilia ni mali ya wananchi na uendelezaji na unyonyaji wa rasilimali hii utafaidisha wananchi kwanza na kwa ruhusa yao (Prior informed Consent Principle) sera ni lazima itamke hilo kinagaubaga.Sera ni lazima ionyeshe kuwa katika ushindani wa soko makampuni ya mafuta na gesi asilia yatapata faida ya halali ( normal retuns) ya uwekezaji wao na kwamba lolote linalozidi litabakia kuwa mali ya wananchi wa Tanzania.

Mkakati wa makampuni ya mafuta na gesi asilia ni kuhakikisha taifa linapata kiduchu na wanasaidia serikali kutoa majibu ya kipato hicho kiduchu. Watanzania hawatakubali tena.

7). Ni lazima tuseme kuwa tunataka utajiri wetu uwe neema kwa wananchi wetu, na siyo laana. Maendeleo yetu yatategemea ni namna gani tunafaidika na utajiri wetu wa maliasili kama gesi asilia. Sera ya Gesi Asilia itujengee imani hiyo. Hii Sera (Rasimu) inapaswa iangaliwe upya na hasa maeneo ya uwazi na uwajibikaji.

 

Kabwe Z. Zitto, Mb Kigoma Kaskazini

Tabora, tarehe 18 Mei 2013

PRESS RELEASE: Shilingi Bilioni 86 zaibwa Wizara ya Nishati/TANESCO, Gridi ya Taifa hatarini

with 36 comments

Shilingi bilioni 86 zaibwa Wizara ya Nishati/TANESCO, Gridi ya Taifa hatarini

Gazeti la The East African la Novemba 24 – 30, 2012 limetoa taarifa kwamba jumla ya dola za kimarekani milioni 54 zimegundulika kuibwa na watumishi waandamizi wa Wizara ya Nishati na Madini na Shirika la TANESCO kupitia manunuzi ya Mafuta ya kuendesha mtambo wa Umeme wa IPTL. Gazeti hili limenukuu taarifa ya ukaguzi kutoka kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Tanzania (Controller and Auditor General). Taarifa hiyo inasema kuna kikundi (racket) ambacho kazi yake kubwa ni kujifaidisha binafsi na mpango wa umeme wa dharura kupitia manunuzi ya Mafuta mazito ya IPTL.

Itakumbukwa kwamba toka mwaka 2011 kumekuwa na shinikizo lililotolewa na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma, Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini na Waziri Kivuli wa Nishati na Madini kwamba zabuni za ununuzi wa mafuta ya kuendesha mpango wa umeme wa dharura na mchakato mzima wa manunuzi ya mafuta haya ufanyiwe uchunguzi wa kina (forensic audit).

Katika mkutano wa 3 wa Bunge la Kumi (April 2011) niliuliza swali Bungeni kuhusu kashfa hii ya ununuzi wa mafuta ya kuendesha mtambo wa IPTL na baadaye tarehe 16 Aprili 2011 nilimwomba Spika airuhusu Kamati ya Nishati na Madini kufanya uchunguzi kuhusu kashfa hii. Kamati ya Nishati na Madini chini ya aliyekuwa Mwenyekiti ndugu January Makamba ililitaka Bunge kuazimia kufanyika kwa uchunguzi kuhusu suala hili kwenye Taarifa yake ya mwaka 2011 iliyowasilishwa Bungeni mwezi Aprili mwaka 2012. Waziri Kivuli wa Nishati na Madini ndugu John Mnyika katika Hotuba yake ya Bajeti ya Wizara hiyo mwaka 2011 alipendekeza kufanyika kwa uchunguzi kuhusu kashfa hii pia. Juhudi zote hizo hazikuzaa matunda.

Kipindi hicho kiwango kilichokuwa kinahojiwa kuibwa ni shilingi bilioni 15 tu. Taarifa ya The East African kama walivyonukuu kutoka kwenye taarifa ya CAG inaonyesha fedha zilizoibwa ni shilingi bilioni 86.

Zabuni za kununua mafuta ya kuendesha umeme wa dharura zimekuwa zikitolewa bila kufuata utaratibu wa zabuni kwa mujibu wa Sheria ya manunuzi. Hivi sasa kila mwezi Tanzania inatumia dola milioni 70 kununua mafuta ya kuendesha mitambo ya umeme. Fedha hizi zinatoka Hazina na sehemu ndogo kutoka TANESCO. Wakati fedha hizi bilioni 112 zinachomwa kila mwezi kununua mafuta mazito na dizeli ya kuendesha mitambo ya umeme, Taarifa za kitaalamu zinaonyesha kwamba Bwawa la Mtera hivi lina kina cha maji chini ya kiwango kinachotakiwa na uzalishaji wa umeme ni asilimia 20 tu ya uwezo (installed capacity). Iwapo TANESCO wataendelea kutumia zaidi maji yaliyopo Mtera, Mitambo itashindwa kazi na Gridi nzima itasimama maana Mtera ndio nguzo kuu ya Gridi ya Taifa. Hali hii ni hatari sana kwa uchumi na ulinzi na usalama wa Taifa. Kimsingi Gridi ya Taifa ipo hatarini kutokana na kiwango cha Maji kilichopo Mtera hivi sasa na kuendelea kupungua kwa kina hicho cha maji.

Wananchi wanapaswa kuelezwa kinaga ubaga nini kinaendelea katika sekta ndogo ya umeme hapa nchini;

1.      Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali kuhusu zabuni za manunuzi ya Mafuta ya kuendesha mitambo ya umeme wa dharura iwekwe wazi na ‘racket’ inayosemekana kuiba jumla ya shilingi bilioni 86 ionyeshwe na hatua za kisheria zichukuliwe mara moja na bila kuchelewa.

2.      Waziri wa Nishati na Maadini auleze umma hali yalisi ya sekta ya umeme nchini, uzalishaji wa umeme upoje, hali ya maji katika bwawa mkakati la Mtera na nini hatma ya mitambo ya IPTL, kesi zake na utekelezaji wa mapendekezo ya Bunge kuwa kesi za kampuni hii zimalizwe nje ya mahakama. Pia Taifa lielezwe Mpango wa Dharura wa umeme unakwisha lini maana muda uliotolewa na Bunge mwezi Agosti mwaka 2011 tayari umekamilika. Waziri aeleze hatua agni amechukua baada ya kukabidhiwa taarifa na CAG kuhusu maafisa waandamizi wa Wizara waliohusika na wizi wa shilingi bilioni 86 za kununua mafuta ya IPTL.

3.      Waziri wa Fedha na Uchumi aueleze umma ni kiwango gani cha fedha Hazina imetoa kununua mafuta ya kuendesha mitambo ya umeme wa dharura kati ya Mwezi Novemba mwaka 2011 na Oktoba mwaka 2012 na kama taratibu zote za zabuni zilifuatwa na pale ambapo hazikufuatwa ni hatua gani PPRA wamechukua dhidi ya waliokiuka sheria ya manunuzi na kuleta hasara ya mabilioni ya fedha kwa Serikali.

 

Kabwe Zuberi Zitto, Mb

Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni na Waziri Kivuli wa Fedha

Dar es Salaam. Novemba 25, 2012