Posts Tagged ‘Taarifa ya CAG’
Tamko la Kiongozi wa chama cha ACT Wazalendo ndg. Zitto Kabwe kuhusu Ripoti ya CAG mwaka 2013/2014
Tamko la Kiongozi wa chama cha ACT Wazalendo ndg. Zitto Kabwe kuhusu Ripoti ya CAG mwaka 2013/2014
1) Taarifa nyingine ya CAG imetoka, kwa mujibu wa Katiba ya JMT na kwa mujibu wa sheria za nchi. Taarifa hii imechelewa kutolewa kulingana na mabadiliko ya Ratiba za Bunge ambapo hapo awali taarifa ilikuwa ikitoka mwezi Aprili na kuwezesha kuchangia katika mchakato wa Bajeti ya nchi. Taarifa ya mwaka huu na ile ya mwaka Jana imetoka wakati wa Bunge la Bajeti na hivyo Bajeti ya Serikali haijazingatia hoja za ukaguzi ili kuboresha mfumo wa matumizi ya fedha za umma. Ni vema utaratibu wa zamani wa ripoti kutolewa mwezi Aprili urejewe ili wabunge waweze kutumia ripoti hizo wakati wa kamati katika kujadili makadirio ya Bajeti za Wizara mbalimbali.
2) Taarifa kama miaka iliyopita bado sio nzuri. Mapato mengi ya Serikali bado yanapotea. Uk. 53 wa Taarifa unaonyesha kuwa mizigo inayoingizwa nchini kupita kwenda nchi jirani zinazotumia bandari zetu hubakia nchini na kuingizwa sokoni hivyo kukwepa kodi. Mwaka 2013/2014 mizigo ya transit iliyobaki nchini kiudanganyifu ilikuwa zaidi ya bidhaa 6000 kwa mujibu wa Taarifa ya CAG. Hivyo kodi ya tshs 836 bilioni haikulipwa kwa mizigo hiyo sawa sawa na 10% ya makusanyo yote ya kodi za ndani. Tshs 836 bilioni ilipotea mwaka 2013/14 peke yake. Wakati hili linatokea Serikali ipo ukata mkubwa na kushindwa kuendesha miradi yake mbalimbali. Fedha iliyokwepwa idara ya forodha peke yake inalipa Madeni yote ya wakandarasi wa barabara wanaoidai TANROADS na riba kulimbikizwa kila mwaka. Fedha hii ingelipa Madeni yote ya mfuko wa PSPF wanayoidai Serikali. Fedha hizi zingeweza kulipia miradi 2 mikubwa nchini ya BVR na vitambulisho vya Taifa ambayo inasuasua kutokana na ukata.
Natoa wito kwa CAG kwanza kuweka wazi orodha ya bidhaa hizo zilizobakia nchini na kuingizwa nchini bila kulipa kodi. Vile vile CAG aweke wazi wafanyabiashara wote walioagiza bidhaa hizi na vyombo vya kiuchunguzi vichukue hatua za kuwashtaki wafanya biashara hawa mara moja.
Natoa wito kwa Kamati ya Bunge ya PAC kuwaita mara moja maafisa wa TRA kujieleza mbele ya kamati kuhusu suala hili na kuandaa taarifa maalumu bungeni ili kuanika uoza huu unaopoteza mapato mengi sana ya Serikali.
3) CAG kaonyesha kuwa kuna ubadhirifu mkubwa sana kitengo cha maafa cha ofisi ya Waziri Mkuu ambapo tshs 163 billioni za chakula cha maafa hazikukusanywa katika kipindi cha miaka 5 iliyopita. Huu ni kama mrija wenye wastani wa tshs 32 bilioni kuchotwa kwa kisingizio cha chakula cha maafa kwa wananchi. Kwa malezo ya CAG ni kwamba Watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu wamekula fedha za chakula cha misaada. Maana hakuna uthibitisho wa kuwa mahindi yaliyogawanywa na taarifa kutolewa na Wakala wa Akiba ya Chakula (NFRA). Kitengo cha maafa ofisi ya PM kimekuwa mrija wa wizi wa fedha za umma, wizi ambao umekuwa ukifanyika bila ya kugunduliwa kwa miaka 5 sasa. ACT Wazalendo inaisihi Kamati ya Bunge ya PAC kufanya uchunguzi maalumu kwenye kashfa hii ya tshs 163 bilioni katika Ofisi ya Waziri Mkuu na Wakala wa Hifadhi ya Chakula ( NFRA).
4) ACT Wazalendo inalitaka Bunge kuchukua stahiki dhidi ya Wizara ya Ujenzi kufuatia ripoti ya CAG kuonyesha kuwa Wizara ilidanganya Bunge katika kupitisha Bajeti ya tshs 252 bilioni ambapo kati yake tshs 87 bilioni ziliibiwa au matumizi yake kutoeleweka.
5) ACT Wazalendo inampongeza CAG kwa kuendelea na zoezi la kisheria la kukagua mahesabu ya vyama vya siasa. Hii inaweka misingi ya uwajibikaji kuanzia kwenye vyama vya siasa, taasisi muhimu sana katika ujenzi wa demokrasia. Vyama vya siasa vichukulie ripoti ya CAG kama changamoto ya kutoa kwanza kibanzi kwenye macho yao ili kuwa na ‘ moral standing’ ya kupambana dhidi ya ubadhirifu wa fedha za umma nchini.
Zitto Kabwe
Kiongozi wa Chama ACT Wazalendo
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI Shilingi bilioni 620 za Deni la Taifa hazina maelezo
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Shilingi bilioni 620 za Deni la Taifa hazina maelezo
Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ametoa taarifa yake ya mwaka 2011/2012 na kuonyesha kuwa kuna skandali kubwa sana katika akaunti ya Deni la Taifa. Nanukuu
‘Uhakiki wa mchanganuo wa madeni ya Taifa kama ulivyokuwa tarehe 30 Juni, 2012 ulibaini kuwepo kwa marekebisho ya deni ya shilingi 619,803,554,183.91 ambayo uongozi haukuweza kutoa maelezo ya kuridhisha.’ (Taarifa ya CAG, Ripoti ya Serikali Kuu 2011/2012 uk 158). Mwisho wa Kunukuu
Katika Taarifa yake hiyo CAG anaendelea kuonyesha kuwa Deni la Taifa linazidi kukua na mwaka unaoishia mwezi Juni 2012 deni lilikuwa kwa asilimia 17 kutoka mwaka unaoishia mwezi Juni 2011.
Kukosekana kwa maelezo ya kuridhisha kuhusu zaidi ya nusu trilioni za Deni la Taifa ni jambo linalopaswa kutiliwa mashaka makubwa, kuchunguzwa na kupata majawabu stahiki. Tafiti mbalimbali duniani zinaonyesha kuwa kuna mahusiano makubwa sana kati ya Deni la Taifa la utoroshaji wa fedha kwenda kwenye mabenki ya ‘offshore’. Katika kitabu cha ‘Africa’s Odious Debts: How Foreign Loans and Capital flight bled a continent’ kilichoandikwa mabwana Leonce Ndikumana na James Boyce imeonekana kwamba Deni la Taifa huchochea utoroshwaji wa Fedha kwenda kuficha nje ya Tanzania.
Mabilioni haya kwenye akaunti ya Deni la Taifa yanashtusha sana. Kambi ya Upinzani Bungeni kwa miaka miwili mfululizo imekuwa ikitaka ukaguzi maalumu kwenye akaunti za Deni la Taifa lakini Serikali imeshindwa kufanya hivyo. Nikiwa Mwenyekiti wa Kamati ya PAC pia nimemtaka CAG afanye ukaguzi huu maalumu.
Kambi ya upinzani Bungeni ilisema hivi katika Bajeti yake kivuli 2012/13:
DENI LA TAIFA
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inasikitika kwa serikali kuendelea kutengeneza madeni kwa Taifa kwa kuendelea kukopa zaidi kwa matumizi ya kawaida ya serikali. Wakati Serikali inasisitiza kwamba Deni letu linastahmilika, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali anaonyesha mashaka makubwa sana kutokana na kasi ya kukua kwa Deni la Taifa. Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali inaonyesha kuwa Deni la Taifa linazidi kuongezeka kwa asilimia 38% kutoka shilingi trillion 10.5 mwaka 2009/2010 hadi shilingi trillion 14.4 mwaka 2010/2011. Kwa mujibu wa Waziri wa Fedha Deni la Taifa limefikia shilingi trillion 20.3 mpaka ilipofika mwezi Machi mwaka 2012. Ukisoma taarifa ya Mwezi wa Mei 2012 ya Benki Kuu ya Tanzania, Deni la Taifa sasa limefikia shilingi trillion 22.
Mheshimiwa Spika, Suala hapa sio ustahmilivu wa Deni kama inavyodai Serikali bali ni kwamba tunakopa kufanyia nini? Bajeti ya Mwaka 2012/13 inayopendekezwa inaonyesha kwamba Serikali itakusanya shilingi trilioni 8.7 kama makusanyo ya ndani na itatumia shilingi trilioni 10.6 kama matumizi ya kawaida. Ni dhahiri kwamba sehemu ya mikopo ambayo serikali inachukua sasa itakwenda kwenye matumizi ya kawaida. Hatutaki mikopo kwa ajili ya matumizi ya kawaida ya posho, kusafiri, magari nk. Tuchukue mikopo kuwekeza kwenye miradi itakayokuza uchumi na kuzalisha kodi zaidi. Bajeti inaonyesha kwamba Serikali itakopa shilingi takribani trillion 5 mwaka 2012/13. Serikali ikubalikutekeleza mapendekezoya Kambi ya Upinzani ya kuimarisha ukusanyaji wa kodi na kupanua wigo wa kodi katika maeneo muhimu kama sekta ya madini na mawasiliano, kuzuia misamaha ya kodi, kutokomeza ukwepaji kodi, na kuepuka matumizi mabaya ili kuepuka madeni yasiyo ya lazima.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inapenda kusisitiza kwamba Bunge lifanye ukaguzi maalumu kuhusu akaunti ya Deni la Taifa ili kuweza kubaini ukweli kuhusu ustahmilivu wa Deni na mikopo ambayo Serikali inachukua kama inakwenda kwenye Maendeleo na miradi ipi na kama miradi hiyo ina tija. Vilevile tumependekeza kwamba Mikopo yote ambayo Serikali inachukua iwe inapata idhini ya Kamati ya Bunge ya Fedha na Uchumi au Bunge litunge sharia ili kiwango cha juu cha kukopa ambacho Serikali haipaswi kuvuka. Kuiacha Serikali inaendelea kukopa bila mpango ni kuliweka Taifa rehani na kupeleka mzigo wa kulipa madeni haya kwa kizazi kijacho. Hatuwezi kukubali Wazee wetu waishi maisha yao, waishi maisha yetu na pia wakope maisha ya watoto wetu. Mwisho wa kunukuu.
Kambi ya Upinzani inarejea kutaka ukaguzi maalumu kuhusu akaunti za Deni la Taifa na maelezo ya kina ya Serikali kuhusu shilingi 620 bilioni ambazo hazina maelezo kwenye Deni la Taifa. Hatuwezi kukaa kimya kuona Watanzania wanabebeshwa madeni ambayo kimsingi ni madeni bandia yanayotajirisha watu wachache wenye uwezo na ujasiri mkubwa wa kuiba, kupora nakufisidi hazina ya Taifa letu.
Kabwe Zuberi Zitto,Mb
Waziri Kivuli Fedha na Uchumi